SERIKALI ya Tanzania, imeanza kuondoa changamoto ya ukata wa fedha, katika Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura), baada ya Mfuko Mkuu wa Hazina kuupaa wakala huo Sh. 172 bilioni, kwa ajili ya kutatua changamoto ya barabara kwenye majimbo. Anaripoti Jemima Samwel.DMC…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 1 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma na Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Ummy Mwalimu, baada ya Mbunge wa Igalula mkoani Tabora (CCM), Daudi Venant, kulalamika ufinyu wa bajeti ya Tarura.
Akijibu malalamiko hayo, Ummy amesema, nje ya fedha zilizotengwa katika Mfuko wa Barabara kwa ajili ya Tarura, kwa mwaka wa fedha wa 2021/2022, Serikali kupitia hazina imetoa Sh. 172 bilioni.
Amesema fedha hizo zimetolewa ili kupunguza kilio cha wabunge, dhidi ya ukata wa fedha katika Tarura.
“Kwa mara ya kwanza Serikali imesikia kilio cha wabunge, sababu fedha za Tarura zilikuwa zinatoka katika mfuko wa barabara, lakini tumepata fedha Sh. 172 bilioni kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina,” amesema Ummy.
Ummy amesema katika mgawo wa fedha hizo, kila jimbo litapatiwa Sh. 500 milioni, zitakazokwenda katika ofisi za Tarura za maeneo yao, kwa ajili ya ujenzi wa barabara.
“Kwa sababu fedha hizi tumezipata haraka haraka na bajeti zimeshapitishwa na kamati za halmashauri , tumetumia maamuzi ya jumla ambapo kila jimbo tunapeleka Sh. 500 milioni, kwa Tarura kwa ajili ya ujenzi wa barabara,” amesema Ummy.
Ummy amesema matumizi ya fedha hizo, yatapangwa na mabaraza ya madiwani ya halmashauri kwa kushirikiana na wabunge.
“Wabunge mtaamua kama Sh. 500 milioni, kujenga kilomita moja ya barabara ya lami au kujenga kilomita 10 ya barabara ya udongo kuwa changarawe. Tumeiweka hii chini ya uamuzi wa mabaraza ya madiwani kuamua,” amesema Ummy .
Aidha, Ummy amesema Wizara ya Fedha na Mipango, inaendelea kufanyia kazi kilio cha wabunge kuhusu Tarura kuongezewa bajeti.
“Na hii ndiyo kazi ya Rais Samia Suluhu Hassan, amesikia kilio chenu na Waziri wa Fedha na Mipango (Dk. Mwigulu Nchemba) ananiambia bado anaangalia angalia,” amesema Ummy.
Leave a comment