SERIKALI imeahidi kukiwezesha Chuo cha Bahari (DMI), cha jijini Dar es Salaam kwa miundombinu bora na vifaa vya kisasa vya kufundishia ili kiweze kuwa na viwango vya kimataifa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Ahadi hiyo ilitolewa leo Jumanne jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Atupele Mwakibete, wakati akifungua kongamano la kwanza la uchumi wa bluu.
Kongamano hilo lililoandaliwa na DMI ni la kwanza kufanyika nchini kuhusu uchumi wa bluu na maudhui yake ni ‘Kuibua fursa zitokanazo na bahari kwa maendeleo ya taifa’.
Alisema eneo kilipo chuo hicho Posta Dar es Salaam ni dogo sana hivyo serikali inaangalia uwezekano wa kutenga eneo kubwa kwenye Mkoa wa Pwani kwaajili ya kupanua shughuli za chuo hicho.
Alisema kwa kuanza serikali imeshatenga Sh bilioni moja kwaajili ya ununuzi wa mfumo wa kufundishia ma nahodha wa meli inayofahamika kama Stimulators.
“Niliwahi kutembelea hiki chuo hivi karibuni na kwa kweli nilijionea mwenyewe miundombinu ilivyo chakavu lakini mkakati uliopo ni kukiwezesha kuwa cha kisasa na kitakuwa na majengo yenye viwango na kwa kuwa wana maeneo makubwa Mkoa wa Pwani itakuwa kazi rahisi kwetu ,” alisema Mwakibete
Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya DMI, Ernest Bupamba, aliiomba serikali iiangalie DMI kwa jicho la huruma ikizingatiwa kuwa ndicho chuo pekee kinachotoa mafunzo ya bahari hapa nchini.
Alisema chuo hicho ndicho pekee kinazalisha rasilimali watu inayohitajika kwenye uendeshaji wa uchumi wa bluu hivyo iwapo kitawezeshwa kwa vifaa na majengo kitatoa mchango mkubwa kwenye kufikia malengo yaliyowekwa kwenye uchumi huo.
Aliishukuru serikali ya visiwa vya Shelisheli kwa namna ambavyo imeisaidia Tanzania katika kupambana na vitendo vya uvuvi haramu kwenye bahari yake.
Alisema mara kadhaa viongozi wa serikali hiyo wamekuwa wakiwasiliana na serikali ya Tanzania kila wanapoona wavuvi haramu na ksiha vyombo vya usalama kwenda kuwakamata na kuwafikisha kunakohusika kwa hatua za kisherkia.
“Ni mara nyingi sana Sheli sheli imekua msaada mkubwa kwa Tanzania kwa sababu kule watu wamekuwa wakijaribu kuendesha uvuvi haramu lakini kila wakijaribu wanatupigia simu na serikali inachukua hatua haraka sana na imesaidia kwa kiasi kikubwa,” alisema
Kaimu Mkuu wa chuo hicho, Tumaini Gurumo alisema kwa mwaka chuo hicho kinazalisha mabaharia 100 ambao wanakidhi soko la ndani na wengine kwenda kufanya kazi nje ya nchi.
“Soko la mabaharia ni kubwa sana sisi tunazalisha 100 kwa mwaka ambao wanakidhi mahitaji ya ndani na wengine wanakwenda kufanyakazi nje ya nchi, vijana wachangamkie fursa hii kwasababu inafedha za kutosha na ajira yake siyo ya kuhangaika,” alisema Dk. Tumaini
Leave a comment