MGODI wa Barrick Bulyanhulu uliopo mkoani Geita umefanikiwa kuboresha miundombinu ya elimu, afya na maji kutokana na fedha za kusaidia huduma za kijamii (CSR) ikiwa ni sehemu ya kusaidia jamii inayozunguka mgodi huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Geita … (endelea).
Baadhi ya miradi iliyotekelezwa wilayani humo ni kujengwa kwa shule ya awali na msingi ya kisasa ya Kharumwa inayomilikiwa na Halmashauri ya Nyang’hwale, katika kitongoji cha Butalanda, inayofundisha masomo kwa mchepuo wa kingereza ambapo fedha za CSR zilizotolewa na Barrick Bulyanhulu kufanikisha mradi huo ni Sh. 300 milioni.
Miradi mingine ambayo fedha za CSR zimechangia kuifanikisha ni ujenzi wa bwalo la chakula katika shule ya Sekondari ya Msalala, iliyogharimu Sh. 94,720,000, ukarabati wa madarasa matatu ya Sh. 25,491,200 pamoja na ujenzi wa madarasa mawili katika sekondari ya Nyijundu kwa gharama ya Sh. 20 milioni.
Pia fedha hizo zimefanikisha miradi ya ujenzi wa hosteli ya wasichana katika shule ya sekondari ya Mwingiro, kwa Sh. 115,858,200, ujenzi wa maabara, Sh. 100 milioni, ujenzi wa bwalo la chakula katika sekondari ya Nyang’hwale kwa gharama ya Sh. 114,818,000 na ukarabati wa vyumba vitatu vya madarasa kwa Sh. 18,043,200.
Barrick hawakuinshia hapo pia wamejenga zahanati ya Lushimba kwa Sh. 70,676,275 na ujenzi wa nyumba ya watumishi katika zahanati hiyo kwa Sh. 25,731,650. zahanati ya Lushimba ambayo itawaondolea wananchi adha ya kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kupata huduma za afya.
Akiongea kuhusiana na miradi hiyo inavyoendelea kuboresha maisha ya wananchi wakati wa ziara ya viongozi wa Barrick Bulyanhulu, walipotembelea miradi hiyo, Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Nyang’hwale, Leonard Mgema, alisema fedha za CSR zimeleta faraja kubwa kwa wananchi na kuwezesha maisha yao kuendelea kuwa bora.
“Kuwepo kwa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu jirani na wilaya yetu kumeipa heshima wilaya yetu, kwani kupitia fedha za CSR ambayo kwetu sisi tunayahesabu kama mapato ya ndani imetufanya kutekeleza miradi mingi ya Elimu, Afya na Maji na mingine mingi,” alisema Mgema.
Alisema ujenzi wa shule ya mchepuo wa kiingereza kumeondoa adha ya watumishi na wafanyabiashara wa eneo hilo waliokuwa wanahangaika kuwapeleka watoto wao maeneo ya mbali kupata elimu pia jambo la kufurahisha shule nyinginezo za Serikali zimezidi kuimairishiwa miundo mbinu na kuwezesha watoto kuendelea kupata elimu katika mazingira rafiki.
Naye Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari ya Msalala, Mpuya Charahani, alitoa shukrani kwa uongozi wa halmashauri ya Nyang’hwale na mgodi wa Barrick Bulyanhulu kwa kuboresha miundo mbinu ya shule hiyo kupitia fedha za mfuko wa CSR.
Baadhi ya wananchi wanaoishi wilayani Nyang’hwale walieleza kuwa wanaendelea kufurahia uboreshwaji wa huduma mbalimbali za kijamii katika maeneo yao kutokana na fedha zinazotolewa na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, kupitia halmashauri ya wilaya hiyo.
Meneja Mkuu wa Mgodi wa Bulyanhulu, Cheick Sangare akiambatana na ujumbe wa maofisa waandamizi wa mgodi huo, walitembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa fedha za kusaidia huduma za kijamii (CSR) zinazotolewa kwa Halmashauri ya Nyang’hwale.
Sangare, amewakikishia wananchi wa Nyang’hwale, kuwa mgodi wa Barrick, upo kwa ajili ya kuhakikisha jamii inanufaika na faida inayotokana na mauzo ya dhahabu pia wataendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuchangia kuleta maendeleo kwa wananchi na aliahidi kuwa changamoto mbalimbali alizokutana nazo katika ziara hiyo zitafanyiwa kazi na kupatikana suluhisho.
Leave a comment