MBUNGE wa Jimbo la Bumbwini, Muhammed Amour Mohammed (CUF), amesema kuwa serikali imekuwa ikitoa majibu mepesi kwa maswali yanayoulizwa na serikali. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Mohammed ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Mei 2019 bungeni wakati akiuliza swali la nyongeza kuwa, inasikitisha kwa serikali kutoa majibu mepesi ambayo hayaendani na maswali yanayoulizwa na wabunge.
Ni baada ya kujibiwa swali la msingi ambalo aliliuliza kwa kulielekeza kwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako.
Awali katika swali la msingi la mbunge huyo, alitaka kujua nini tamko la serikali kuhusu matokeo ya kidato cha nne kuwa mabaya kwa kipindi kirefu bila kupatiwa ufumbuzi wowote?
Pia alitaka kujua, ni juhudi zipi za makusudi ambazo serikali inakusudia kuchukua ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi hao.
“Matokeo ya mitihani ya kidato cha nne yamekuwa mabaya kwa kipindi kirefu, na hali hiyo hii haijapatiwa ufumbuzi wowote. Je, nini tamko la serikali kuhusiana na matokeo ya kidato cha nne kuwa mabaya kwa kipindi kirefu?
“Ni juhudi zipi za makusudi ambazo serikali inakusudia kuchukua ili kupandisha hali ya ufaulu wa wanafunzi hao?” amesema.
Akijibu swali hili William Ole Nasha, Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia amesema, ufaulu wa wanafunzi katika kidato cha nne umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka ambapo katika mwaka 2018, watahiniwa waliofaulu ni asilimia 78.36 ukilinganishwa na asilimia 77.09 katika mwaka 2017 asilimia 70.35 ya mwaka 2016 na asilimia 67.91 ya mwaka 2015.
Amesema kuwa, serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuongeza ufaulu katika ngazi mbalimbali za elimu, hatua hizo ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia kwa kujenga na kufanya ukarabati mkubwa wa miundombinu katika shule.
Na kwamba, katika mwaka wa fedha 2018/19 zaidi ya Sh.93.8 Bilioni zimetumika katika uboreshaji wa miundombinu ya shule ya 588 (Misingi 308 na Sekondari 285) yakiwemo madarasa 1,190 mabweni 222 na vyoo 2,141, mabwalo 76 na nyumba 99.
Leave a comment