RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Serikali haijafunga mipaka kuuza mazao nje ya nchi, bali inataka kuwe na mfumo wa ununuzi, uuzaji na usafirishaji wa mazao yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Pia amerejea agizo lake kwamba sasa hivi wakulima hawana ruhusa ya kuuza mazao nje wenyewe bila kuwa na mfumo wowote wa kiserikali.
Rais Samia ametoa agizo hilo leo tarehe 8 Agosti wakati akifungua sherehe za maonesho ya wakulima nane nane yaliyofanyika kitaifa katika viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya.
Amesema mfumo huo mpya wa uuzaji mazao nje utaiwezesha serikali kufahamu kiasi cha mazao kinachouzwa nje na fedha inayopatikana ili kudhibiti wafanyabiashara wasiowaaminifu.
“Nataka wizara ya kilimo kwa kushirikiana na TAMISEMI, TRA na Uhamiaji muweke mfumo wa pamoja kusimamia biashara ya mazao nje ya nchi ili wakulima wetu wanufaike na kilimo wanachofanya,” amesema.
Amesema uzoefu uliopo sasa ni kwamba magari yanatoka nchi jirani yanaingia moja kwa moja kwenye mikoa, wilaya hayauliziwi na yanakwenda mpaka kwa wakulima kununua mazao.
“Na pale wanakwenda kulipa fedha zetu za ndani mawakala wanagaiwa pesa mipakani huko wanaingia kukusanya mazao yetu kwa fedha za ndani, haya ni maazao ambayo tunaweza kuuza kwa fedha za nje.
“Kwa hiyo tukiweka mfumo mzuri wa ununuaji, tukithibiti magari yale kwenda moja kwa moja kwa mkilima tutakuwa tunajua tunauzaje, na tunalipwaje.
“Ndio maana mwaka huu nikakupa fedha nyingi waziri (Hussein Bashe) ili NFRA inunue mazao kwa wakulima tuweke stoo, watu nje wakitaka kununua wanunue kwetu serikali badala ya kwenda kwa mkulima,” amesema.
Aidha, amemuagiza Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe kukaa na wizara ya fedha kuona namna ya kupunguza bei ya mbolea.
Katika hotuba yake Bashe alisema Serikali imepanga kutumia Sh bilioni 200 kutoa ruzuku kwenye mbolea ambayo inatarajiwa kusambazwa zaidi ya tani 650,000 kwa wakulima katika msimu ujao.
Alisema mbolea hiyo itauzwa kati ya Sh 65,000 hadi 70,000.
Leave a comment