RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na Rais wa China, Xi Jinping. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mazungumzo hayo, yamefanyika leo Jumatatu, tarehe 21 Juni 2021.
Rais amempongeza, Rais Samia kwa kuchukua kijiti cha uongozi na kumpa pole kwa kuondokewa na Rais Hayati John Pombe Magufuli.
Hayati Magufuli alifariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam na mwili wake, kuzikwa 26 Machi 2021, nyumbani kwao Chato, Mkoa wa Geita.
Katika mazungumnzo hayo, Tanzania na China zimekubaliana kukuza ushirikiano katika nyanja za uchumi, utamaduni na ushirikiano wa Kimataifa.

China imeahidi kufungua zaidi soko lake kwa bidhaa za Tanzania pamoja na kuongeza uwekezaji hususan katika sekta ya viwanda.
Aidha, kupitia mazungumzo hayo, China imeahidi kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya sita katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika nyanja mbalimbali.
Rais Samia, ametumia fursa ya mazungumzo hayo kutoa salamu za pongezi kwa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) kwa kuadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwake na ameahidi kudumisha uhusiano wa kidugu na kihistoria uliopo kati ya Chama hicho na Chama cha Mapinduzi (CCM).
Taarifa ya mazungumzo hayo, imetolewa na Jaffar Haniu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu.
Leave a comment