USHIRIKIANO kati ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ACT-Wazalendo katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika tarehe 28 Oktoba 2020 umeanza kushika kasi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Viongozi wa vyama hivyo katika nyakati tofauti, wametoa kauli za ushirikiano katika Uchaguzi wa Urais wa Tanzania na Zanzibar, ubunge na udiwani huku Chadema kikitoa kauli rasmi ya kumuunga mkono Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad.
Jana Jumatano tarehe 7 Oktoba 2020, Mgombea mwenzas wa Rais kupitia Chadema, Salum Mwalimu alimnadi Mgombea Ubunge wa Tunduru Kaskazini mkoani Ruvuma, Ado Shaibu kupitia Chama cha ACT-Wazalendo.
Mwalimu alifanya tukio hilo katika mkutano wa kampeni wa uliofanyika jimboni humo.
“Kama ni Ado lazima tumhakikishie maslahi yake ya ushindi yanakuaje hatuwezi kumuacha, tutakwenda na Ado lakini kamanda wetu huyu tusimuache lazima tuweke akiba mbele ya safari huko,” alisema Mwalimu.
Mwalimu ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Chadema Zanzibar, ameutaka uongozi wa Chadema na wafuasi wa chama hicho katika Jimbo la Tunduru Kaskazini kumuunga mkono Ado, kwa kuwa anaushawishi mkubwa kwa wananchi ikilinganishwa na mgombea wao.
“Mnajua nani tunayetamani atuongoze, kwenye vyama vyetu hivi kuna wagombea udiwani na ubunge ili vyama vyetu hivi yako maeneo ambayo tukicheza vibaya tunaipa nguvu CCM lakini tukicheza vizuri CCM anakosa, hawezi akashidna hata akiongeza kura za wizi,” amesema Mwalimu.
Jumapili ya tarehe 4 Oktoba 2020, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alitangaza kumuunga mkono Maalim Seif katika kinyang’anyiro cha Urais Zanzibar, huku akisema mgombea wao Said Issa Mohammed ameridhia kujitoa katika uchaguzi huo.
Hali kadhalika Maalim Seif, katika mkutano wake wa kampeni visiwani Zanzibar uliofanyika hivi karibuni alitangaza rasmi kumuunga mkono, Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chadema, Tundu Lissu.
Vile vile, Lissu alipofanya mkutano wake wa kampeni mkoani Kigoma katika Jimbo la Kigoma Mjini, aliwataka wafuasi wa Chadema kumchagua mgombea mwenye nguvu katika jimbo hilo.
Zitto Kabwe, Mgombea Ubunge wa Kigoma Mjini kupitia ACT-Wazalendo, anaonekana kuwa na ushawishi mkubwa katika uchaguzi wa jimbo hilo.
Leave a comment