ROSTAM Aziz, mfanyabiashara mkubwa na mbunge wa zamani wa Igunga, Tabora ametoa mashine kubwa 25 za vitakasa mwili wote ili kukabili virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Rostam amekuwa mfanyabiashara mkubwa wa kwanza Tanzania kutoa msaada wa namna hiyo, tangu kuingia ugonjwa wa corona nchini.
Mfanyabiashara huyo pia ametoa barakoa 70,000 kwa ajili ya madaktari na wauguzi wanaohudumia wagonjwa wa corona nchini, ikiwa ni hatua ya wakuwalinda.
Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo tarehe 16 Aprili 2020, mbele ya Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam katika viwanja vya Karimjee.
“Ugonjwa huu hauna tiba, tiba pekee ni usiupate,” amesema Rostam na kuongeza “pamoja na kutoa sanitaiza hizo kubwa, nimeongeza mchango wangu kwa wauguzi, najitolea barakoa 70,000 ili madaktari na manesi wanaohatarisha maisha yao, waweze kujilinda.”
Akizungumza mbele ya Makonda, Rostam amesema Watanzania wanapasa kuchukua tahadhari zaidi kuliko kipindi chochote tangu ugonjwa huu uingie nchini.
“Hivi sasa ni wazi tahadhari hizo inabidi tuzizingatie zaidi kuliko wiki ama wiki mbili zilizopita. Leo hii kwa mara ya kwanza nimevaa hii kitu kinaitwa barakoa. Na hii nimetengenezewa na mama yangu.
“Unachukua shuka ama foronya, unakata kitambaa unakunja mara mbili unaweka na pamba tayari umetengeneza barakoa,” amesema Rostam.
Mfanyabiashara huyo ametoa wito kwa wafanyabiashara wengine nchini kuungana na serikali katika kukabilia corona, na kwamba haihitaji kuwa mfanyabiashara mkubwa ili kuisaidia serikali dhidi ya corona.
“Naomba wafanyabiashara wenzangu.. hili si suala la seikali peke yake, hata Marekani, China wafanyabiashara wamesaidia serikali zao, na sisi Tanzania wafanyabiashara lazima wajitokeze kusaidiana na serikali kwasababu huu ni mzigo mzito,” amesema.
Pia amekumbusha ujumbe wa Rais John Magufuli alioutoa tarehe 22 Machi 2020, kwamba kila mmoja anapaswa kuchukua tahadhari kubwa ikiwa ni pamoja na kunawa mikono mara kwa mara, kutopeana mikono na tahadhari zingine.
Katika makabiano hao, Makonda amesema watu ama ndugu wanaotaka kwenda Dar es Salaam kwa ajili ya kuwatembelea, “huu sio muda muafaka.”
Amesema, hata wale wa Dar es Salaam wanapaswa kubaki ndani ya jiji hilo ili kupunguza kueneza virusi hivyo.
“Wapo ndugu wanatamani kuja Dar kutembelea ndugu, naomba radhi wananchi wote wa Dar es Salaam ambao hawakubali watu kuwatembelea baki huko huko, naungana nao. Acha kusalimiana salimiana, hali imebadilika.
“Tuwaacheni wa Dar tupambane kwanza na hili janga, na wewe wa Dar es Salaam kama huna sababu za kwenda mkoani, baki hapa hapa tupambane na huu ugonjwa, usiende kuwapelekea ugonjwa huko,” amesema.
Leave a comment