MKUU wa Mkoa wa Shinyanga, Sophia Mjema ametoa wito kwa wanawake kuiga mfano wa kikundi cha Mshikamano kujitosa kwenye uchimbaji wa madini ya dhahabu kwani siyo kazi inayotakiwa kufanywa na wanaume pekee. Anaripoti Paul Kayanda, Shinyanga …(endelea).
Mshikamano ni kikundi kinachoundwa na jopo la wanawake wachimbaji wa madini ya dhahabu katika Halmashauri ya Msalala Wilayani Kahama mkoani Shinyanga.
Akizungumza katika kongamano la wanawake lililoandaliwa na Mbunge wa Msalala, Idd Kassimu (CCM) kuelekea kwenye maadhimisho ya sherehe ya Siku ya Wanawake Duniani, Mjema amesema tayari Rais Samia Suluhu Hassan amekwisha fungua mlango hivyo wanawake wajitokeze kwenye shughuli ya uchimbaji wa madini.
Amesema wanawake wasipochagua kazi wataweza kujikwamua kiuchumi hasa ikizingatiwa Serikali na viongozi wote wapo nyuma yao.
Aidha, amesisitiza hatua kali zitachukuliwa kwa wanaume wanaobeza shughuli za wanawake kwa lengo la kuwakwamisha.
“Natoa rai kwa kikundi cha Mshikamano kwamba ikitokea kuna shida ya kukwamishwa na wanaume watoe taarifa haraka… mama anapochimba ni sawa na mwanaume kwani kikundi hicho kimefuata taratibu zote kwa mujibu wa sheria za madini katika kukabidhiwa na serikali eneo lenye mfumuko wa dhahabu ‘Rush’,” alisema.
Mjema amesema kazi ya uchimbaji wa dhahabu ni ngumu na siyo kazi rahisi ndiyo maana imezoeleka kuwa wanaume pekee ndiyo wanaoweza kazi ngumu ya uchimbaji.
“Lakini akina mama hawa wameungana na kuanzisha kikundi chao na wamethubutu na sasa wanachimba Dhahabu,” amesema.
Mjema amesema kundi hilo la kinamama kupitia muungano wao wa kikundi cha Mshikamano kwa sasa wamepewa na serikali eneo lenye mfumuko wa Dhahabu (RUSH) ili wakusanye maduhuli ya serikali, huko kijiji cha Nyamishiga Kata ya Lunguya Halmashauri ya Msalala.
“Kwa kweli nawapongeza wanawake kwa hatua ya kuthubutu kupambana na wanaume katika maombi ya usimamizi wa RUSH na wakashinda kwa kweli kwa kipindi kifupi wanawake hawa tangu wakabidhiwe Rush hiyo mpaka sasa wamekusanya kodi ya sereikali zaidi ya shilingi milioni 200,” alipongeza RC Mjema.
Aidha, Mwenyekiti wa Rush hiyo, Semeni John amesema changamoto kubwa ni mfumo dume wa kudhani kuwa wanawake hawawezi kusimamia maeneo ya uchimbaji.
“Baada ya tamko la Waziri wa Madini, Dk. Dotto Biteko kwamba wamama wapewe Rush hiyo walijitokeza akinababa waliodhani wakinamama hao hawawezi wakaanza kuwavamia kwenye maeneo yao wakishinikiza yakatwe katwe jambo ambalo hawakufanikiwa kulingana na msimamo wa Waziri,” amesema.
Kwa upaende wake Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Festo Kiswaga naye alipongeza hatua ya kikundi hicho cha wanawake kwa kupambana mpaka hatua ambayo wamepata usimamizi wa Rush hiyo.
Aidha ameapa kukisimamia kikundi hicho kisivamiwe na watu ambao wanajiita ni wenye mitaji.
“Ninaendelea kukaribisha vikundi vya wanawake kuomba usimamizi na kupata leseni,” amesema.
Leave a comment