MKUU wa mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel amewataka wakazi wa mkoa huo kuipokea filamu ya Royal tour ambayo inatarajiwa kuonyeshwa tarehe 18 mwezi huu katika jengo la biashara la Rock City Mall jijini humo na kutembelea vivutio vilivyopo nchini na mkoa huo ili kukuza pato la nchi. Anaripoti Sophia George, Mwanza… (endelea).
Mhandisi Gabriel amesema filamu hiyo inayotarajiwa kutazamwa na watu zaidi ya 1000 inalenga kuunga mkono juhudi na kazi kubwa iliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kukuza na kuutangaza utalii wa Tanzania utamaduni pamoja na vivutio vilivyopo nchini.
Aidha, Mkuu huyo wa mkoa amevitaja vivutio vilivyopo katika mkoa huo kuwa ni pamoja na jiwe maarufu la Bismark, Hifadhi ya Taifa ya kisiwa cha saa nane.
Vingine ni makumbusho ya kabila la wasukuma la Bujora, mti wa kunyongea, Gunzert house, Ziwa victoria, mnara wa samaki, mahakama na gereza la kwanza kipindi cha ukoloni, makaburi ya wahanga wa meli ya mv Bukoba na mnara wa mwalimu JK Nyerere uliopo Igoma.
Katika hatua nyingine Mhandisi Gabriel amewataka maofisa rasilimali watu kuhudhuria mkutano wa siku tatu unaolenga kuwakumbusha wajibu wao pindi wanapotekeleza majukumu yao ga kazi ili wafanye kazi zao kwa weledi.
Kwa upande wake mjumbe wa Kamati Tendaji ya Umoja wa Maafisa Rasilimali na Utawala Tanzania (HRAOAT), Monica Andrew amesema mkutano huo utasaidia kuwaweka sawa maafisa rasilimali na kuwakumbusha namna ya kufanyaa kazi kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Leave a comment