MKUU wa Mkoa wa Arusha, John Mongela leo tarehe 11 Juni, 2022 amethibisha kutokea kwa mapigano katika wilayani Ngorongoro tarafa ya Loliondo ambapo askari polisi mmoja amepoteza maisha kwa kupigwa mshale jana alasiri. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari jijini humo, Mongela amesema alasiri ya jana askari mmoja aliuawa kwa kupigwa mshale na kundi la watu wenye silaha ambalo lilitokea na kutaka kuathiri zoezi la uwekaji mipaka wilayani humo.
“Pamoja na kauli nzuri ya Waziri Mkuu jana, alasiri kulitokea zoezi hilo, lakini mpaka sasa kwenye maeneo yetu yote hatuna majeruhi kwenye hospitali zetu na vituo vya afya, ingawa tumeona kwenye mitandao, kuna picha zinatolewa.
“Bahati mbaya sana baadhi ya picha ni za miaka mingi iliyopita, kuna ambazo zimetambulika ni za miaka mitatu minne imepita,” amesema Mongela.
Aidha, ametoa wito kwa mtu yeyote mwenye jeraha na chochote ambacho anadhani limesababishbwa na vyombo au mamlaka za Serikali ajitokeze ili apate huduma kwa sababu huo ndio muelekeo wa serikali.
“Serikali yetu ni serikali ya utawala wa sheria, misingi ya utawala bora, tungependa suala la upotoshaji lisiendelee. Kwa sababu tunafanya jambo ambalo ni la kimaendeleo kwa mustakabali wa wananchi wetu na jamii zetu na masilahi mapana ya nchi yetu,” amesema Mongela.
Pia amewataka wananchi wa Tarafa ya Loliondo wilaya ya Ngorongoro kuwa watulivu na kusikiliza maelekezo ya serikali katika zoezi la uwekaji mipaka.
Leave a comment