RAIS Samia Suluhu Hassan amesema suala la posho ya kufundishia (teaching allowance) kwa walimu ni mzigo mkubwa kwenye kapu la serikali hivyo atakwenda kuangalia uwezo wa nchi na kuona atafanya nini. Anaripoti Gabriel Mushi, Morogoro … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo baada ya Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA), Tumaini Nyamuhokya kumuomba kuwarejeshea walimu mpango wa posho hiyo ambayo imesitishwa kwa muda mrefu.
“Mabango ni mengi lakini kuna neno dogo limekuwa likinipa shida kwenye mabango hayo ya walimu… linaitwa teaching allowance, wameweka kwenye mabango yao.
“Ilikuwepo siku za nyuma lakini katikati kikapotea na kufifia, leo wametukumbusha, ikikupendeza usisahau watumishi walimu katika hilo,” amesema Rais Nyamhokya wakati akitoa hotuba ya kumkaribisha Rais Samia kuhutubia katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani leo tarehe 1 Mei 2023.
Aidha, Rais Samia ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo yaliyofanyika kitaifa katika uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro, amesema suala hilo amelibeba.
“Suala la teaching allowance tumelichukua, unajua walimu na sekta ya afya ni jeshi kubwa, kwa hiyo allowance za walimu hata zikiwa ndogo ukiweka kwa pamoja ni mzigo mkubwa kwenye kapu la serikal hivyo tutakwenda kuangalia uwezo wa nchi alafu tuone tutafanya nini lakini tumelibeba,” amesema Rais Samia.
Leave a comment