RAIS Samia Suluhu Hassan amewatoa hofu waajiriwa katika taasisi na mashirika ya umma yatakayofutwa kutokana na sababu mbalimbali kwamba watahamishiwa kwenye mashirika mengine kwani Serikali haiwezi kupoteza nguvu kazi yao. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hatua hiyo imekuja baada ya Ofisi ya msajili wa hazina kufanya uchambuzi na kubaini taasisi ambazo majukumu yanashabihiana na nyingine ambazo kwa sasa majukumu yake yamepitwa na wakati huku nyingine utendaji wake unalegalega.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 19 Agosti 2023 wakati akifungua kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wa mashirika ya umma kinachofanyika jijini Arusha.
“Katika maboresho tunayoyafanya hakuna nguvukazi au ajira itakayopotea, wote ambao wapo kwenye mshirika aidha watamezwa kwingine au kutakuja mashirika mengine yenye maana sasa kuliko wakati yalipoanzishwa. Naomba msihofu msiogope mabadiliko yaliyopo,” amesema.
Amesema Serikali inafanya hivyo kwa sababu, takwimu zinaonesha asilimia 17 ya ajira nchini inatolewa na taasisi, mashirika na wakala hivyo haiwezi kuyaondoa ili ajira zipotee.
Amesema mpango huo utaipunguzia serikali gharama za uendeshaji na kuongezea ufanisi.
“Tumeambiwa mashirika haya ndio nguzo kuu ya maendeleo ya serikali, nguzo ya uchumi wa serikali. Yakizalisha wa vizuri Serikali inapata tija na kufanya makubwa zaidi, yakiwa mzigo inarudisha nyuma maendeleo ya serikali,” amesema.
Leave a comment