WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Rais Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuongoza mazishi ya Waziri Mkuu Mstaafu Hayati Edward Lowassa yanayotarajiwa kufanyika Wilayani Monduli mkoani Arusha Jumamosi tarehe 17 Februari 2024. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Awali Rais Samia alitangaza siku tano za maombolezo ya kitaifa ambapo bendera zitapeperushwa nusu mlingoti kuanzia tarehe 10 Februari 2024.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Jumapili wakati akitoa taarifa ya ratiba ya mazishi ya kiongozi huyo, Ofisi Ndogo ya Waziri Mkuu Oysterbay, Dar es Salaam.
Amesema katika kipindi cha siku tano za maombolezo, Taifa litaendelea na shughuli za umma na kijamii sambamba na kushirikiana na wanafamilia katika ratiba ya msiba kama ilivyoandaliwa na kamati ya mazishi ya Kitaifa na wanafamilia.
Amesema kabla ya mazishi hayo mwili wa Hayati Lowassa unatarajiwa kuagwa katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam na Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.
Amesema Jumanne tarehe 13 Februari 2024 mwili wa Hayati Lowasa unatarajiwa kuangwa na viongozi na wananchi katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Waziri Mkuu amesema Jumatano tatehe 14 Februari mwili wa Hayari Lowasa utapelekwa katika Kanisa la KKKT Azania Front kwa ajili ya ibada takatifu na kuaga.
Amesema Alhamisi tarehe 15 Februari mwili wa Hayati Lowassa utasafirishwa hadi jijini Arusha ambapo viongozi na wananchi watapata fursa ya kuaga katika viwanja vya Sheikh Amri Abeid.
Waziri Mkuu huyo mstaafu alifariki jana Jumamosi wakati akipatiwa matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam na tangazo la kifo chake lilitolewa na Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango.
Leave a comment