RAIS Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa mkutano wa kumbukumbu ya Maalis Seif Sharif Hamad unaotarajiwa kufanyika kwa muda wa siku mbili kuanzia tarehe 5 hadi 6 Novemba mwaka huu huko Visiwani Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea)
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 2 Novemba, 2021 na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Muda ya Maalim Seif Foundation, Ismail Jussa, mbali na Rais Samia, pia mkutano huo utahudhuriwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman.
Jussa amesema mkutano huo ambao maudhui yake ni “Maalim Seif, umoja na Maridhiano katika Ujenzi wa Zanzibar na Tanzania mpya” utafanyika katika ukumbi wa Golden Tulip Hotel, Zanzibar.
“Tayari watu mashuhuri kutoka ndani na nje ya nchi wamethibitisha kuhudhuria wakiwemo watakaohutubia kwa njia ya video kutoka nje ya nchi.
“Miongoni mwao ambao wamethibitisha kuzungumza ni Rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Amani Karume, Waziri mkuu mstaafu, Jaji mstaafu Joseph Warioba, Aliyekuwa waziri wa sheria Kenya, Martha Karua, Makamu wa Rais wa Taasisi ya Friedrich Naumann Foundation for Freedom ambaye alikuwa Waziri wa Sheria wa Ujerumani, Sabine Shanarrenberger pamoja na wasomi na watafiti wakiwemo Prof. Issa Shivji, Prof. Rwekaza Mukandala na Jenerali Ulimwengu,” amesema.
Amesema viongozi wa kitaifa wa vyama vya siasa, dini, asasi za kiraia na mabalozi wan chi za nje wanaowakilisha nchi zao hapa nchini pia watahudhuria.
Leave a comment