RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amezihimiza nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Masharik (EAC), kuboresha sekta ya kilimo, ili uzalishaji wa mazao uongezeke na kuondoa utegemezi wa chakula kutoka nje. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Rais Samia ametoa wito huo leo Alhamisi, tarehe 21 Julai 2022, katika mkutano wa kawaida wa 22 wa wakuu wa nchi za EAC, uliofanyika jijini Arusha, baada ya kuulizwa swali nini kifanyike ili nchi hizo ziweze kujilisha zenyewe.
Mkuu huyo wa Tanzania, amesema mageuzi hayo yanabidi yaende sambamba na utekelezaji wa miradi ya maji, ili kuimarisha kilimo cha umwagiliaji wakati wa ukame.
“Ardhi peke yake haitoshi, tunatakiwa tuangalie maji, namna ya kumwagilia ardhi. Miradi ya maji ni mizuri namna gani tutavuna maji ya mvua tupate maji tumwagilie mashamba. Suala lingine kuangalia namna ya kupata fedha na pembejeo za kisasa,” amesema Rais Samia.
https://youtu.be/qd_QI_q822E
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameshauri wakulima wasaidiwe fedha, pamoja na kuwajengea uwezo wa kutunza mazao yao kabla na baada ya kuvuna.
“Vyanzo vya fedha, wakulima waweze kusaidiwa kubadilisha kilimo chetu Afrika Mashariki, lingine tunapoteza sana mazao kipindi cha mavuno na kabla ya mavuno ambapo mazao yako shambani. Kwa kweli baada ya kuvuna tunapoteza tunatakiwa tuwe na mbinu ya kuvuna mazao yetu,” amesema Rais Samia.
Leave a comment