MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, amemkabidhi Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ripoti ya matumizi ya fedha zilizotolewa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kati ya Januari na Machi, 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Ripoti hiyo, imebaini upungufu kadhaa ikiwemo, baadhi ya taasisi kama vile Wakala wa Barabara Tanzania, (Tanroads) na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kufanya malipo mara mbili kwa kazi moja au kuchelewa kutumia fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya malipo ya kazi husika.
CAG Kichere, amekabidhi ripoti hiyo leo Alhamis, tarehe 1 Julai 2021, Ikulu ya Chamwino, jijini Dodoma.
Ukaguzi huo, ulifanyika baada ya Rais Samia, kumwagiza CAG na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), tarehe 28 Machi 2021, wakati akipokea taarifa ya CAG kwa mwaka 2019/ 2020.
“…lakini upotevu mkubwa unatokea huko, na wewe mwenyewe CAG umesema hali si shwari na hatua za haraka zinahitajika.”
“Naomba nitoe agizo kwako na Takukuru, naomba nenda pitia na Gavana wa benki yupo hapa, pitieni fedha zote zilizotoka katika kipindi cha Januari mpaka Machi mwaka huu, zilizokwenda kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo tunataka kuziona,” alisema Rais Samia siku anatoa maagizo.
Akiwasilisha taarifa hiyo, CAG Kichere amesema, katika ukaguzi uliofanyika imebainika fedha zilizotolewa BoT katika kipindi hicho zilifuata taratibu zote, isipokuwa baadhi ya malipo yaliyokuwa yanatoka Hazina Kuu kwenda katika taasisi mbalimbali za Serikali yalibainika kuwa na mapungufu.
“Mapungufu hayo ni pamoja na baadhi ya taasisi kama vile Wakala wa Barabara nchini (Tanroads) na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kufanya malipo mara mbili kwa kazi moja au kuchelewa kutumia fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya malipo ya kazi husika,” amesema Kichere
Vilevile, CAG Kichere amesema, yamejitokeza mapungufu ambapo baadhi ya makandarasi waliotoa huduma kucheleweshewa malipo yao hali inayosababisha madeni ya makandarasi kuwa makubwa kutokana na riba ambayo ni mzigo kwa Serikali.
Amesema, mapungufu mengine ni pamoja na kuwepo kwa miradi ambayo haikupangwa na hivyo kufanya malipo nje ya bajeti ya Serikali.
Leave a comment