FATMA Karume, Wakili na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) anaongoza mawakili wenzake upande wa mashtaka kupinga uteuzi wa Mwanasheria Mkuu Serikali (AG), Dk. Adelardus Kilangi uliofanywa na Rais John Magufuli. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi, Mawasiliano na Uenezi, ACT -Wazalendo ndiye aliyefungua madai hayo ambayo yameanza kusikilizwa leo tarehe 7 Februari mwaka 2019.
Madai hayo yamefunguliwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ambapo Ado anapinga utaratibu uliotumika kuteuliwa Dk. Kilangi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Jopo la Majaji wanaosikiliza kesi hiyo ni pamoja na Jaji Kiongozi Dk. Dk Eliezer Felishi, Dk Benhajj Masoud na Jaji Luvada.
Kwenye kesi hiyo namba 29 ya mwaka 2019 Ado ameiomba mahakama mambo matatu ;- Mahakama itamke kuwa Rais Magufuli amevunja Katiba kwa kumteua Dk Kilangi kuwa Mwanasheria Mkuu, mahakama itamke kuwa Dk. Kilangi amevunja Katiba kwa kukubali kuteuliwa na Rais Magufuli kinyume na Katiba na pia mahakama itamke kuwa uteuzi huo sio halili na ni uvunjifu wa Katiba ya Nchi.
Mahakama imeipa serikali siku 14 kujibu mashtaka ya Ado. Shauri hilo limeahirishwa mpaka tarehe 22 Februari mwaka huu kwa ajili ya kusikiliza majibu ya serikali juu ya mashaka hayo.
Rais Magufuli alimteua Dk. Kilangi kushika wadhifa huo tarehe Mosi Februari 2018. Kabla ya kuteuliwa kwake, alikuwa Mkurugenzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu cha Arusha pia alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Shughuli za Mkondo wa Juu wa Mafuta.
Leave a comment