WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania, Profesa Adlof Mkenda amewataka wadhibiti ubora wa elimu nchini kutumia vifaa vya kisasa kuboresha mazingira ya elimu nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Profesa Mkenda amesema hayo leo Jumanne, tarehe 5 Aprili 2022 jijini Dar es Salaam wakati akizindua zoezi la usambazaji wa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) kwa maafisa ythibiti ubora wa shule na maafisa elimu kata pamoja na taasisi zetu za kielimu.
Amesema vifaa vinavyozinduliwa ni kompyuta 3,354 ambapo kati ya hizo Laptop ni 1637 na Deskotop kompyuta ni 1717, printer 12, projector 12 na internet switches 12 vikiwa vimenunuliwa na Serikali pamoja na wadau wa Elimu ili kuunga jitihada za awamu ya Sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hasan ya kuwekeza kwenye Elimu.
Profesa Mkenda amesema, kati ya kompyuta zinazozinduliwa, laptop 1,337 zinatokana na program Covid Recovery ambao ni mradi wa kuboresha mazingira Salama ya kujilinda na maambukizi ya virus vya korona.
Amesema komputa hizi zitagawiwa kwa maafisa uthibiti ubora na maafisa elimu kata ili kuboresha utendaji kazi wao Komputa Mpakato na Tehama zitasaidia kurahisisha utendaji wa Kazi; utunzaji na uchakataji wa taarifa na Takwimu.
Waziri huyo amesema, vifaa hivyo vitapunguza gharama ya viandikia kwakuwa taarifa zinaweza kupatikana katika nakala laini. Komputa zitarahisisha Mawasiliano baina ya maaafisa na wadau wa Elimu.
Amesema, kundi jingine la vifaa vinajumuisha Desktop komputa 1717, Laptop 300, Printer 12, Projector 12 na Internet Switches 12. Vifaa hivi vimetolewa na Shirika la “Digital Pipeline” la nchini Uingereza na vitasambazwa katika shule zetu za Msingi, Sekondari na vyuo vya ualimu.
“Niwaombe tukavitumie vifaa hivi vizuri ili vilete tija katika nyanya ya kufundishia na kujifunzia,” amesema Profesa Mkenda
Amesema wizara imekwisha gawa vifaa vya Tehama ikiwa ni kompyuta za mezani (Desktop) 1,120, kompyuta za mkononi au mpakato (laptop) 413 na projekta 186 kwenye vyuo vyote vya ualimu vya Serikali.
Profesa Mkenda amesema, vifaa hivi viligawiwa kwa vyuo vyote 35 vya Ualimu, ili kusaidia kupunguza uwiano wa matumizi ya kompyuta kwa wanachuo kutoka wanachuo 28 kwa Kompyuta 1 (28 :1) hadi kufikia wanachuo 2 kwa Kompyuta 1 (2 :1) vyuoni.
Amesema lengo la usambazaji wa vifaa hivyo ni kuhakikisha kuwa uandaaji wa walimu unakuwa wa kisasa na unaendana na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Mthibiti Mkuu wa Ubora wa Shule Kanda ya Kusini, Michael Cheyo amesema, ”hiki ni kitendea kazi muhimu sana na kinatufanya kwenda na wakati. Tunapofanya tathimini ndani ya siku 14 mteja au mwenye shule awe amepata ripoti, sasa kupitia hiki tutafikia shule nyingi, kufanya kazi kwa ubora.”
Aidha, ameomba mafunzo yatolewe ya kutumia kompyuta hizo ili kuwaongezea ujuzi ili tuweze kuwa na ujuzi wa kuvitumia.”
Naye Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Anders Sjoberg ambao ni miongoni mwa wafadhili wa vifaa hivyo amesema, Sweden itaendelea kuwa pamoja na Tanzania katika kuboresha sekta ya elimu nchini kwenye maeneo ya kujifunza na kufundishia.
Awali, Aloyce Kamamba, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii amesema, kazi yao ni kushauri na kufuatilia shughuli zinazofanywa na Serikali.
“Suala la kuwa na vifaa ni suala moja na suala la vifaa kwenda kuleta matokeo chanya ni jambo jingine. Moja ya silaha kubwa ya elimu ni wathibiti ubora na kama waziri ukiwatumia vizuri hawa elimu itakwenda kupaa na niombe kazi za wathibiti ubora zifanyiwe kazi na kwa ubora kabisa,” amesema,
Leave a comment