MBUNGE wa Ubungo, jijini Dar es Salaam nchini Tanzania, Profesa Kitila Mkumbo, ameiomba Serikali ifanye upanuzi wa Barabara ya kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma, ili kupunguza ajali zinazotokea kutokana na wingi wa magari. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Prof. Mkumbo ametoa ombi hilo leo Ijumaa, tarehe 31 Machi 2022, jijini Dar es Salaam, katika ibada ya kuuaga mwili wa aliyekuwa Profesa wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Honest Ngowi na wa dereva wake, Innocent Mringo, waliofariki kwa ajali ya gari iliyotokea maeneo ya Mlandizi, mkoani Pwani, tarehe 28 Machi 2022.
Mbunge huyo wa Ubungo, amesema barabara hiyo inaongoza kwa kuwa na ajali zinazopoteza maisha ya Watanzania.
“Hawa wote wamefariki kwa ajali na bahati mbaya sana takwimu zinaonesha Tanzania kwamba ajali ndiyo chanzo kikubwa cha vifo vya watu. Na kwa kweli Barabara ya Dar es Salaam hadi Dodoma, ni moja ya barabara zenye ajali nyingi sababu ina magari mengi,” amesema Prof. Mkumbo na kuongeza:
Prof. Mkumbo amesema “napenda kuisihi Serikali ione haja ya kuwa na mradi mkubwa wa kupanua barabara ya Dar es Salaam hadi Dosoma, ili kuepusha ajali zinazotokea.”
Prof. Mkumbo amesema marehemu Prof. Ngowi alitumia taaluma yake kuuelimisha umma kuhusu masuala ya uchumi.
“Mwenzetu alivuka daraja la mwanataaluma wa kawaida akawa mhadhiri wa umma, ndiyo maana hata sisi hatukusoma naye tulifahamiama naye kwa karibu sababu ya usomi wake kwa umma mpaka wamachinga wanamfahamu. Anatufundisha wanataaluma haitoshi kuwa wa darasani tungependa kuona uprofesa wako wananchi wananufaika nao,” amesema Prof. Mkumbo.
Aidha, Prof. Mkumbo ameipa pole familia ya Prof. Ngowi na Mringo.
Prof. Ngowi na dereva wake, Mringo, walifariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea katika barabara hiyo, ambapo gari yao iliangukiwa na kontena.
Prof. Ngowi alipata ajali hiyo akiwa safarini kuelekea mkoani Morogoro kikazi, akitokea Dar es Salaam.
Leave a comment