CHAMA cha ACT-Wazalendo kimezuiwa kufanya mkutano wake wa ndani na Jeshi la Polisi mkoa wa Kipolisi Temeke kutokana na kukosa kibali. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Chama hicho kilipanga kufanya mkutano wa ndani wa kuwajengea uwezo viongozi wake wa kata, katika ukumbi wa Hoteli ya Sunrise iliyoko Temeke jijini Dar es Salaam ambapo Maalim Seif Shariff Hamad, Mshauri wa ACT-Wazalendo, alitarajiwa kufungua mkutano huo.
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 24 Agosti 2019 na Ray Matata, Katibu wa Itikadi na Uenezi ACT-Wazalendo mkoa wa Dar es Salaam wakati akizungumza na MwanaHALISI Online kwa njia ya simu.
Matata amesema asubuhi ya leo askari polisi walifika katika ofisi za chama hicho, Kata ya Azimio na kuwaeleza viongozi waliokuwepo hapo kwamba hawaruhisiwi kufanya mkutano huo kwa sababu hawana kibali cha polisi.
“Tulikuwa na tukio la uzinduzi wa matawi na mkutano wa ndani wa kichama wa kuwajengea uwezo viongozi wa matawi, mshauri wa chama angekuja kufungua, wamekuja polisi na kuzuia wakisema kwamba mkutano wa ndani unatakiwa kuwa na kibali, wamesema hatuna kibali zimekuja gari za kutosha zimezuia ofisi ya Kata ya Azimio,” amesema Matata.
Aidha, Matata amesema wanaendelea kufuatilia suala hilo, na kisha watatoa taarifa kamili kwa umma.
Leave a comment