MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) umeiomba serikali iunde tume huru kwa ajili ya kuchunguza madai ya baadhi ya polisi katika Kituo cha Polisi Mafinga mkoani Iringa, kunyanyasa watuhumiwa wakiwa mahabusu. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 24 Agosti 2019 na Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa kupitia ukurasa wake wa Twitter.
“Leo ni siku ya 3 tangu alipokamatwa Mhariri wa maudhui wa Watetezi TV, Joseph Gandye, tunaiomba Serikali iunde tume maalumu kuchunguza tuhuma zinazomkabili na si kulitegemea jeshi la polisi ambao ndio walalamikiwa,” ameomba Olengurumwa na kuongeza.
“Tunahitaji kamati huru ya uchunguzi dhidi ya madai ya polisi kunyanyasa mahabusu. Ni kinyume na haki watuhumiwa kuchunguza tuhuma zao wenyewe. Mwacheni huru Gyande.”
Ombi hilo limekuja ikiwa ni siku tatu zimepita tangu Joseph Gandye, Mhariri wa Maudhui wa Watetezi TV inayomilikiwa na THRDC kukamatwa na Jeshi la Polisi mkoani Iringa kwa tuhuma za kuchapisha habari za uongo dhidi yake.
Gandye ambaye ni Mhariri wa Maudhui wa Watetezi TV inayomilikiwa na THRDC tarehe 22 Agosti 2019 alipokea wito wa kujisalimisha katika Kituo cha Polisi cha Urafiki jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu tuhuma zinazomkabili, kutoka kwa Askari Polisi aliyejitambulisha kwa jina la Godfrey Mkude.
Baada ya kuhojiwa, Alfajiri ya tarehe 23 Agosti 2019 alisafirishwa na polisi kuelekea mkoani Iringa, mahala anakotuhumiwa kutenda kosa hilo. Na alipowasili, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, ACP Juma Bwire alisema mtuhumiwa huyo atarudia tena kuhojiwa na Jeshi la Polisi.
Wakili wa THRDC, Chance Luoga anayefuatilia suala hilo, amesema Gandye anatarajiwa kuhojiwa leo, na kwamba kama zoezi hilo litakamilika atafuatilia masuala ya dhamana.
Leave a comment