BENKI ya NMB kwa kushirikiana na Vodacom na Google, wamezindua kampeni ya ‘Miliki Simu, Lipa Mdogo Mdogo’, inayowezesha watanzania wa kipato cha chini na kati kumiliki simu janja (smartphone). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kampeni hiyo inalenga kuhakikisha watanzania wengi zaidi wanakuwa sehemu ya uchumi wa kidijitali kwa maendeleo endelevu.
Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo jijini Dar es Salaam Ijumaa Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa Benki ya NMB, Filbert Mponzi amesema NMB imeingia makubaliano na kampuni ya Vodacom ili kurahisisha upatikanaji wa mikopo ya simu janja hizo.
Amesema katika kuwezesha urahisi wa malipo mteja atalipa kianzio cha Sh 20,000 kisha kulipa kuanzia Sh 900 tu kwa siku pia atachagua kufanya malipo kwa wiki au mwezi.
“Mteja anaweza kujiunga na huduma hii kupitia menu ya M-Pesa, kisha kufika kwenye duka lolote la Vodacom kuchukua simu yake,” amesema.
Amesema kwa mwaka huu zitatolewa simu milioni moja kwa wateja ambao watakidhi vigezo vya kukopeshwa.
Aidha, ameongeza kuwa ubia huo una tija kwani utafungua uchumi wa kidijitali na kutengeneza fursa za ziada kwa Watanzania.
“Ushirikiano huu utaongeza kasi ya kuleta huduma za kifedha nchini, na unaenda kuongeza nguvu kwenye kampeni yetu ya “Teleza Kidijitali” inayolenga kuwafikia watu wengi nchini na huduma jumuishi za kifedha,” ameongeza.
Mkurugenzi wa Fedha wa Vodacom Tanzania, Hilda Bujiku amesema: “Maoni yetu daima ni kuipeleka Tanzania kwenye ulimwengu wa kidijitali na kubadilish maisha kupitia teknolojia. Hivyo, ushirikiano huu unaenda sambamba na azma yetu ya kuwafungulia wateja wetu fursa zinazobadilisha maisha.”
Leave a comment