AFISA Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna amesema benki hiyo imejipanga kuwainua wanawake kiuchumi na kutambua shughuli zao za uzalishaji mali ili kuwakomboa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ruth amesema hayo leo Alhamisi tarehe 28 Aprili 2022 wakati wa kuorodheshwa rasmi kwa hati fungani ya Jasiri iliyo chini ya NMB katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) jijini Dar es Salaam.
Amesema kiasi cha fedha kilichopo ni Shilingi Bilioni 74.3 zitakazotumika kuwakopesha wanawake na watu wanaofanya biashara zinazohusiana na masuala ya wanawake.
“Azma yetu wakati wa kuanzisha hatifungani hii ni kuboresha maisha ya wanawake na kuinua vipato vyao. Awali tulianza na wazo la kukusanya Sh Bilioni 25 lakini ndani ya wiki sita tangu tulipoizindua Februari 7, 2022 tumefanikiwa kukusanya Sh Bil 74.3, ni zaidi ya mara tatu au asilimia 197 ya malengo tuliyojiwekea,” amesema Zaipuna.
Aidha, kwa wale ambao hawakufanikiwa kununua hatifungani hiyo kabla ya leo, watalazimika kwenda kuzinunua katika Soko la Hisa la Dar es Salaam ambao imeelezwa watapata riba ya asilimia 8.5, na wale wanaotaka kuuza hatifungani zao watalazimika kuziuza hapo hapo DSE.
Akizungumza katika hafla hiyo, mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Lawrence Mafuru alisema NMB wameonesha ujasiri wa hali ya juu kwanza kwa kuja na kitu kipya sokoni lakini pia kuamua kuendelea kuuza hatifungani hata kabla mfumo huo wa kipekee barani Afrika haujasajiliwa rasmi.
“Aliyebuni jina la Jasiri Bond, amekuja na kitu kipya na cha kipekee chenye kuakisi uhalisia wenu kama NMB. Mmeonyesha maana halisi ya kuwa viongozi sokoni. Mmeamua kuja na bidhaa mpya sokoni kijasiri, ni jambo la kupongezwa sana,” amesema Mafuru.
Amebainisha kwamba wana shaka na wazo la kuwalenga wanawake katika hatifungani hii warejee malengo ya Milenia (SDG) lengo namba 5 na 10 ambayo yanaweka wazi kabisa namna ya kumuondolea mwanamke vikwazo vya kiuchumi na kuweka usawa wa kijinsia katika shughuli za kiuchumi na kijamii.
“Hongereni NMB kwa kuonyesha njia, serikali ipo tayari kujifunza kwenu. Jambo hili ni la kwanza katika ukanda huu wa Afrika Mashariki. Nimeambiwa waliochangia kiasi hicho cha zaidi ya Bil 74 ni asilimia 53 ya wanawake ambao ni wanawake 843, ni jambo la kupongezwa,” amesisitiza Mafuru.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa International Finance Corporation (IFC), Frank Ajilore alisema NMB wameonyesha upekee katika soko la fedha kwa kuleta kitu kipya ambacho hakipatikani katika ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.
“Sijaona utaratibu huu popote, ndio maana wazo lilipofika ofisini kwetu tukapambana kuhakikisha mnapata usajili. NMB mmeonyesha kuwajali wanawake, hii ni dhamira ya dhati na ukomavu katika sekta ya kibenki. Ahsanteni NMB kwa kuwajali wanawake,” amesema Frank.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa DSE, Moremi Marwa amesema, “NMB mmeonyesha njia katika ule utaratibu wa kusaidia jamii kupitia sekta ya kibenki. Mnafanya uwekezaji lakini wakati huo huo mnafikiria kusaidia jamii na mazingira.”
Katika Sh Bil 74.3 zilizokusanywa imeelezwa kuwa asilimia 99 ya wawekezaji ni wa ndani na asilimia moja ndio wa nje. Na asilimia 99.9 ya wawekezanji ni wadogo, maana yake inaonyesha kuna fursa nyingi kwa wawekezaji wadogo na asilimia 83 ya wawekezaji wametoka nje ya Jiji la Dar es Salaam.
Leave a comment