KAMPUNI ya kidijitali ya Media Convergency kwa kushirikiana na kampuni ya Meta imezindua mpango wa kuwapatia mafunzo ya kidijitali Watanzania 1000 kutoka katika Mashirika 35 yasiyo ya Kiserikali (NGOs) kwa lengo la kuyawezesha mashirika hayo kuingia kwenye mfumo wa kidijitali. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hatua hiyo imekuja baada ya kubainika kuwa asilimia 95 ya NGO hizo zilizosajiliwa hapa nchini, zinafanya kazi na kutoa huduma kwa kutumia mifumo ya zamani (analojia) badala ya kidijitali.
Akizungumza leo tarehe 28 Aprili, 2022 katika uzinduzi rasmi wa Mradi wa NGOkidijitali uliofanyika jijini Dar es Salaam, Ofisa Mtendaji mkuu wa Media Convergency, Asha Abinallah amesema NGOs hizo 35 zitakuwa katika chini ya uangalizi maalumu kwa zaidi ya miezi sita.
Amesema hatua hiyo itaangazia moja ya mikakati ya Media Convergeny katika ripoti iliyotolewa Julai mwaka jana ambayo ni kukuza mazungumzo, mabadiliko na uhamasishaji wa matokeo chanya.
Aidha, ametoa wito na ombi kwa mashirika hayo yasiyo ya kiserikali na wadau wote katika sekta hiyo kushirikiana nao katika mradi huo.
“Tunaahidi kutoa huduma thabiti zenye ubora wa hali ya juu. Tunaamini kwa pamoja tunaweza kuipeleka Tanzania katika uchumi wa kidijitali uliokomaa katika mapunduzi haya ya nne ya viwanda,” alisema.
Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Kampuni ya Meta ambayo pia ndio inamiliki mitandao mikubwa ya kijamii duniani kama Instagram, Facebook na Whatsap, Desmond Mushi amesema dhumuni kuu la mradi huo uliolenga NGOs ni kuhamasisha mazungumzi, mitazamano na mabadiliko ya kiteknolojia na kidijiti.
Amesema Meta inalenga kusaidia sekta ya mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo yamekuwa washirika katika kuleta matokeo chanya kijamii katika ukanda wa kusini mwa jangwa la Sahara, kujifunza kuongeza matokeo chanya katika kazi zao kupitia matumizi ya majukwaa ya Meta na kutumia teknolojia za kidijitali.
Amesema mradi huo utasaidia NGOs kwenda na kasi ya dunia ya uchumi wa kidijitali katika kipindi cha nne cha mapinduzi ya viwanda.
“Malengo haya yanaungwa mkono na dhamira ya Meta kwa ukuaji wa Tanzani, kwa kutekeleza program zinazosaidia mashirika yasiyo ya kiserikali na sekta ya mabadiliko ya kijamii nchini kwa nia ya kujenga ushirikiano wa kimkakati na washirika wa ndani na wadau wa sera katika nafasi ya mabadiliko ya kijamii,” alisema.
Aidha, Msajili wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Vickness Mayao amesema mradi huo umekuja wakati muafaka hasa ikizingatiwa Serikali nayo imejidhatiti katika matumizi ya dijitali.
Amesema tangu kufanyike mageuzi makubwa ya kidijitali ndani ya ofisi hiyo ya msajili mwaka 2020, kulikuwa na NGOs 12,000 lakini baada ya uhakiki kutokana na usaidizi huo wa kidijitali, zimebakia asasi binafsi 7000 ambazo zipo hai katika utoaji wa huduma.
“NGOkidijitali utasaidia sana mashirika mengi hasa ikizingatiwa asilimia 95 bado yapo kwenye mfumo wa analojia.
“Sababu kuu inayodaiwa kukwamisha mashirika hayo kuhamia dijitali wanadai ni gharama lakini si kweli kwa sababu dijitali ndio mfumo mahsusi katika uendeshaji wa mashirika haya duniani,” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tehama kutoka Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia, Mulembwa Munaku ametoa wito kwa NGOs hizo pamoja na wawakilishi wake kuhakikisha zoezi la ukusanyaji wa anuani za makazi na postikodi zinawafikia ili kurahisha shughuli hizo za kidijitali.
Amesema Tanzania imeendelea kujiimarisha kidijitali kwa kuhakikisha mikoa yote imefikiwa na mkongo wa Taifa wa Mawasiliano wakati nchi nane zinazoizunguka Tanzania nazo zimeunganishwa na mkongo huo.
Amesema nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ndio nchi pekee iliyobaki kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo haijaunganishwa na mkongo huo, hivyo sasa ni muda sahihi kwa NGOs nazo kujiunga na mifumo ya kidijitali.
Aidha, Mmoja wa wadau wa NGOs kutoka Shirika la Global Peace Foundation, Sylvia Mkomwa akizungumza katika uzinduzi huo, ametoa wito kwa watekelezaji wa m,radi huo kuhakikisha wanazingatia miundombinu ya walemavu katika utoaji huduma hizo za kidijitali kwa NGOs
Sylvia ambaye ni Meneja Miradi na Mawasiliano wa Shirika hilo la Global Peace pia amesema; “Tunaamini kuwa mradi huu wa DigitalNGO utakuwa kichocheo cha mabadiliko na mapokeo ya kidijitali kwa mashirika mengi nchini.”
Programu za Meta kwa mashirika yasiyo ya kiserikali pia zimetekelezwa nchini Nigeria na Afrika Kusini kupitia mfululizo wa ushiriki ikiwa ni pamoja na mafunzo, vikao vya kusikiliza na warsha kwa mashirika yasiyo ya kiserikali.
Leave a comment