SERIKALI imeshindwa kufikisha asilimia 50 ya bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara, iliyoidhinishwa na Bunge la Jamhuri kwa mwaka wa fedha 2019/20. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akiwasilisha bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2020/21, leo tarehe 5 Mei 2020, Innocent Bashungwa, Waziri wa Viwanda na Biashara amesema, wizara hiyo ilipokea Sh. 33 Bilioni badala ya Sh. 100 Bilioni kama ilivyoidhinishwa na bajeti.
Fedha hizo zilizotolewa na serikali (33,812,276,737.40) ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ambapo kiasi cha Shilingi 51,500,000,000 kilichotengwa kwa ajili ya maendeleo, hakikutolewa.
“Mheshimiwa Spika; Katika mwaka 2019/2020, Wizara (Fungu 44 & 60) iliidhinishiwa matumizi ya jumla ya Shilingi 100,384,738,648. Kati ya hizo, Shilingi 51,500,000,000 ni za Matumizi ya Maendeleo na Shilingi 48,884,738,648 za Matumizi ya Kawaida.
“…hadi kufikia mwezi Machi, 2020, Wizara ilipokea jumla ya Shilingi 33,812,276,737.40 ambazo ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Aidha, wizara haikupata fedha kwa ajili ya matumizi ya maendeleo,” ameeleza.
Pia amesema, wizara iliidhinishiwa kukusanya jumla ya Sh. 14,300,000 kutokana na uuzaji wa nyaraka za zabuni na marejesho ya mishahara endapo mtumishi ataacha kazi.
“Hadi kufikia tarehe 31 Machi 2020, wizara haikufanikiwa kukusanya kiasi chochote kutoka vyanzo hivyo,” amesema.
Leave a comment