CHAMA cha NCCR-Mageuzi nchini Tanzania kimezindua Ilani yake ya Uchaguzi Mkuu wa Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020, waliyoipa jina la ‘Ilani ya Mwafaka wa Kitaifa’. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ilani hiyo imezinduliwa leo Jumamosi tarehe 5 Septemba 2020 katika Viwanja vya Zakhiem-Mbagala jijini Dar es Salaam.
Akizungumzia ilani hiyo, Elizabeth Mhagama, Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, amesema ilani hiyo imekuja na mwafaka wa hali ya kisiasa iliyoko hivi sasa
“Ilani yetu tumeiita Ilani ya mwafaka wa kitaifa, ni ilani ya mwafaka wa kitaifa na hatutanii tuko sawa sawa na tumekuwa mfano kwa muda wa miaka mingi wa uvumilivu. Kwa hiyo, tumekuja na ilani ya mwafaka wa kitaifa ambayo inalileta taifa letu kuwa moja,” amesema Elizabeth
Amesema endapo chama hicho kitashinda uchaguzi huo na kuunda Serikali yake, itavunja upendeleo wa kisiasa.
“Nia tunayona kile tunachokisema, Ilani hii itatekelezwa kwa kuanza na mwafaka wa kitaifa. Ni jibu la hali ya kisiasa iliyopo hivi sasa, inavunja kisasi na ukabila kwa misingi ya itikadi za siasa zetu. Ni ilani ambayo inavunja upendeleo wa kisiasa ambao tumeushuhudia,” amesema
Amesema, Ilani hiyo imeandaliwa kwa kushirikisha wadau mbalimbali ikiwemo viongozi wa dini, asasi za kiraia na Rasimu ya Katiba Mpya iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa chini ya Mwenyekiti Jaji Joseph Warioba.
“Ilani hii ikiwa na hoja kubwa ya mwafaka wa kitaifa imetokana kwa kuangalia rasimu ya Jaji Joseph Warioba iliyotumia mabilioni ya fedha za Kitanzania lakini haikupatikana kwa sababu ya kukosekana kwa muafaka wa kitaifa,” amesema Elizabeth
Naye Makamu Mwenyekiti NCCR-Mageuzi, Angelina Mutahiwa amesema, chama hicho kitafanya kampeni zake kistaarabu bila matusi.
“Wananchi ni waelewa mno, hawahitaji matusi, wanahitaji maendeleo sio matusi wala kupiga. Sisi tutajikita kwenye hoja za msingi zilizoko kwenye ilani yetu na watu watatuelewa, sisi tuna hoja kubwa ya maridhiano. Sisi tumeshauanzisha ndani ya chama chetu tuna maridhiano,” amesema Mutahiwa.
NCCR-Mageuzi kimemsimamisha Yeremia Kulwa Maganja kugombea Urais wa Tanzania na Haji Ambar Khamis akiwa mgombea wake mwenza ambao wamekabidhiwa Ilani hiyo kwa lengo la kuinadi kwa Watanzania.
Leave a comment