WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, amesema waandishi wa habari na wadau wengine wa tasnia hiyo, bado wana nafasi ya kuendelea kutoa maoni yao juu ya Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, uliowasilishwa bungeni jijini Dodoma, hivi karibuni. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Nape ametoa kauli hiyo kupitia mahojiano yake na kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV, yaliyorushwa jana tarehe 6 Machi 2023, baada ya kuulizwa kama muswada huo umebeba maoni na mapendekezo yaliyotolewa na wadau wa habari kwa ajili ya kuondoa vifungu vinavyokandamiza tasnia hiyo.
Waziri huyo wa habari amesema kuwa, Muswada huo uliopelekwa bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), umebeba maoni na mapendekezo yaliyokusanywa kutoka kwa wadau na Serikali.
“Bahati nzuri baada ya kuwasilishwa bungeni, Bunge kupitia kamati yake inachukua muswada linarudi kwa wanahabari tena. Kwa hiyo wanayo room kusema hiki ndicho tulichokubaliana au sicho tulichokubaliana, halafu baada ya pale inajadiliwa ndani ya Bunge inakuwa sheria,” alisema Nape na kuongeza:
“Kwa hiyo bado iko room ya wanahabari kusema, tunadhani tumekusanya kila jambo tulilokubaliana, lakini bado Bunge litawaita wataenda kutoa maoni yao na sisi tutakuwa na wajibu wa kujibu na tutajieleza na wao watajieleza mwisho wa siku mtunga sheria ni Bunge.”
Leave a comment