ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, amefariki dunia akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Jeshi la Lugalo, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa kifo hicho imetolewa leo tarehe 18 Julai 2023 na familia ya marehemu Jecha, ikiwa ni saa chache baada ya mwenyekiti huyo mstaafu wa ZEC kufariki dunia.
“Kwa masikitiko makubwa tunawatangazia taarifa ya msiba wa mzee wetu aliyekuwa mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi. Taarifa za mazishi tutawajulisha, familia haijapanga bado mazishi yatakuwa saa ngapi,” imesema taarifa hiyo.
Jina la Jecha lilijizolea umaarufu Zanzibar, Tanzania Bara na nje ya mipaka ya nchi, mnamo 2015, baada ya kufuta matokeo ya uchaguzi mkuu visiwani humo, kwa madai haukuwa huru na wa haki na kwama kulikuwa na ukiukwaji mkubwa washeria za uchaguzi.
Hatua ya Jecha kufuta matokeo hayo, iliibua mvutano mkali kati ya ZEC na Chama cha Wananchi (CUF), kilichodai imefanywa kwa hila ili kuzuia ushindi wake katika kiti cha urais, wawakilishi na hata wabunge. Katika uchaguzi huo uliofanyika Oktoba 2015, CUF kilimsimamisha Hayati Maalim Seif Sharif Hamad, kugombea urais wa Zanzibar.
Baada ya kuondoka ZEC, jina la Jecha liliibuka tena Juni 2020, baada ya mwanasiasa huyo kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kugombea urais wa Zanzibar.
Hata hivyo, hakufanikiwa na hatimaye Rais wa sasa wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi, alipitishwa kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa 2020, kisha kushinda.
Leave a comment