OTHMAN Masoud Sharif, Makamu wa Kwanza wa Rais visiwani Zanzibar, ametaja mambo matatu yaliyombeba kuteuliwa katika nafasi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
“Mambo ambayo nadhani yamenisaidia kufika katika nafasi hii ni pamoja na uzoefu katika kazi, kufanya kazi kwa ushirikiano na muumini wa kutaka nchi kuwa mbali zaidi kimaendeleo,” amesema Othman Masoud.
Ametoa kauli hiyo jana Jumanne tarehe 2 Machi 2021, siku ambayo aliapishwa kushika wadhifa huo ikiwa ni siku moja baada ya kuteuliwa na Dk. Hussein Mwinyi, Rais wa Zanzibar.
Uteuzi huo unatokana na kifo cha Maalim Seif Sharif Hamad, kilichotokea tarehe 17 Februari 2021, jijini Dar es Salaam na kuzikwa siku iliyofuata kijijini kwake Mtambwe, Nyali kisiwani Pemba.
Othman Masoud amesema, miongoni mwa mambo anayopenda katika jamii ya Wazanzibari ni umoja kutamalakijambo ambalo alikuwa akipigania Maalim Seif.
“Mimi ni muumini wa umoja kwa sababu naelewa umuhimu wake, ugomvi wa Wazanzibari ni wa kubuni hivyo suala la umoja ni muhimu kwa maendeleo ya Wazanzibari,” amesema.
Kiongozi huo ambaye si maarufu sana katika siasa za Zanzibar amesema, atakuwa bega kwa bega na Dk. Mwinyi kuijenga Zanzibari ili kufikia ndoto yao.
Ujenzi huo utazingatia msingi imara wa maridhiano, kutazama maslahi mapana ya taifa na matarajio ya wananchi.
Amesisitiza, kwamba Zanzibar imetumia muda mwingi kwenye migogoro ambayo haijengi, hivyo kisiwa hicho kushindwa kusonga mbele.
“Sote ni mashahidi tumetumia muda mwingi kwa mambo ambayo hayajatupeleka mbele pale panapostahiki, kwa hivyo kwa kutumia uzoefu nilioupata, nitajitahidi kwa kadri ya uwezo wangu kumsaidia rais kujenga msingi madhubuti, yeye kwa kushirikiana na mzee wetu Maalim Seif waliujenga ukiwamo wa maridhiano,” amesema.
Leave a comment