SHIRIKA la Posta Tanzania (TPC) linamsaka Mkuu wake wa Kitengo cha Usalama, George Mwamgabe anayedaiwa kutoweka kusiko julikana wiki moja iliyopita. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
TPC imefikia uamuzi huo baada ya Mwamgabe kutoonekana ofisini kwake kwa muda mrefu bila ya kutoa taarifa yoyote, ambapo ilimtafuta kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo nyumbani kwake pasipo mafanikio.
Taarifa ya TPC iliyotolewa na Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa shirika hilo, Joseph Ngowi imemtaka Mkuu huyo wa Usalama kuhudhuria kwenye kikao cha nidhamu kilichoitishwa, ambacho kinatarajiwa kufanyika tarehe 1 Novemba 2018 katika ofisi za makao makuu ya TPC, kwa ajili ya kujibu tuhuma zinazomkabili.
Taarifa ya Ngowi inaeleza kuwa, kama Mwamgabe hatahudhuria kikao hicho pamoja na kutotoa taarifa kwa mwajiri wake, TPC itaendelea na kikao hicho ikiwemo maamuzi yake.
Leave a comment