WAKATI Shirika la NIC Insurence likitimiza miaka 60 tangu kuanzishwa kwake limekusudia kufanya mageuzi makubwa kwenye kilimo kwa kutoa bima kwa wakulima na wafugaji. Anaripoti Faki Sosi …(endelea)
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 16 Oktoba, Mkuregenzi wa NIC Dk. Elirehema Doriye amesema kuwa Shirika hilo linakwenda kuwa suluhisho la hasara kwenye kilimo.
NIC ilianzishwa tarehe 16 Oktoba mwaka 1963 baada ya Serikali kuona ombwe la huduma ya bima ambapo wakati huo taifa lilikuwa changa.
Amesema kuwa kutakuwa na bima mbalimbali zitakozokuwa zinawaokoa wakulima pindi watakapopata majanga na kuwarejesha tena shambani endapo atapata hasara.
“Tuna Bima ya mazao endapo mkulima atavuna chini ya kiwango atalipwa kiasi alichowekeza, endapo itanyesha mvua kubwa, au kukawa kuna uhaba wa mvua , mazao kuungua moto… kwa mkulima aliyekata bima atarejeshewa pesa yake aliyowekeza” amesema Dk. Doriye.
Kwa upande wa ufugaji Dk. Doriye amesema kuwa mfugaji atalipwa endapo mifugo yake aliyoikatia bima imekufa au kupata hasara kwenye shughuli hiyo.
Amesema kuwa wakati Shirika hilo linaadhimisha miaka 60 ya kuanzishwa kwake NIC itakuwa na bidhaa na zawadi nyingi kwa wateja wake kwa ajili ya ubora wa miaka 60 ijayo.
Amesema kuwa Shirika hilo litajikita kwenye uendeshaji kwa njia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama). Kutoa huduma za kipekee lakini kuanza matumizi ya teknolojia ya akili bandia (AI).
Dk. doriye amesema kuwa shirika hilo linafikiria kupanua wigo wake kuwa kuanzisha bima itakayowakinga waandishi wa habari na majanga baada ya kufanya mapitio juu ya utaratibu wa vyombo vya habari.
Amesema kuwa awali Shirika hilo lilikuwa likijihusisha na biashara kubwa lakini sasa litashuka chini kwenye biashara ndogondogo na wafanyabiashara wadogo.
Amesema katika kuadhimisha miaka 60 ya kuasisiwa kwa Shirika hilo kutafanyika mambo yafuatayo:- kutoa elemu ya bima kwa wananchi, kufanya matamasha ya michezo ambapo kutapangwa kuchezwa mechi kati ya Waandishi wa habari na wafanyakazi wa NIC, kutoa msaada kwenye afya na wanajamii wanaoishi kwenye mazingira magumu.
“Tutafanya kampeni ya NIC Kitaa tutakwenda mtaani kutoa elimu ya kitaalam kuhusu bima, tutafanya ziara kwenye vyombo vya habari pia tutakuwa tunatoa elimu kwa umma.
Dk. Doriye amesema kuwa shirika hilo limeingia makubaliano ya mashirikiano na timu ya soka ya Yanga ambapo watashughulikia eneo la michezo kuifikia jamii.
Ameongeza kuwa ushirikiano huo hautaishia Yanga bali pia klabu nyingine zitakazofungua milango ya ushirikiano zitapewa nafasi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manejementi ya Yanga, Andrew Mtine amesema kuwa Shirika hilo linafanya kazi zake kwa usanifu Yanga wanajivunia kufanya kazi nao.
Leave a comment