ALIYEKUWA Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Maharage Chande, ameondolewa katika Shirika la Mawasiliano la Tanzania (TTCL) ndani ya muda mfupi, kutokana na mgongano wa kimaslahi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Sababu hiyo imetajwa leo tarehe 26 Septemba 2023 na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, baada ya kumhamisha Chande kutoka TTCL kwenda Shirika la Posta Tanzania.
Rais Samia amesema, amemuondoa Chande TTCL baada ya kugundua ana biashara ndani ya shirika hilo.
“Maharage tumekutoa TANESCO na nikachukulia uzoefu wako kwenye DSTV na kadhalika, nikaona TTCL ingekufaa zaidi. Sasa baadaye nikagundua una biashara ndani ya TTCL na kwa sababu kampuni ile inafanya vizuri na ndiyo maana imemuwezesha kijana yule nae kufanya vizuri , nikasema hapana usiende mahali ambako una biashara itakuwa conflict of interest (mgongano wa kimaslahi),”amesema Rais Samia.
Mkuu huyo wa nchi amesema, amnemchagua Chande kuwa Postamasta Mkuu, kutokana na uzoefu wake katika masuala ya kidigitali.
“Nikaona sasa nikupe Upostamasta Mkuu, mwezi uliopita nilishiriki mkutano wa Posta Afrika pale Arusha, nikakuta Posta yetu wanakwenda kidigitali nikajua hayo ni maeneo yako,” amesema Rais Samia.
Leave a comment