JAMES Bwire, Meya wa Jiji la Mwanza hana urafiki na waandishi wa habari kwa madai wanabagua. Anaripoti Moses Mseti…(endelea).
Pia Bwire ametoa sababu nyingine kuwa, waandishi wanatumwa na hivyo huamua kuchukua picha za video kwa baadhi ya madiwani na kuwaacha wengine.
Hisia hizo ndio zimemsukuma kuwatimuwa waandishi kwenye kikao cha Baraza la Madiwani waliokwenda kuchukua tukio hilo kwa ajili ya habari.
Bwire alitoa amri ya kuwatimua waandishi leo Ijumaa tarehe 18 Januari 2019 kwenye baraza la wazi la halmashauri wakati diwani wa Kata ya Luchelele, Andrew Vicent alipokuwa akichangia kuhusu kata ambazo zimeondolewa kwenye mpango wa ujenzi wa ofisi licha ya kuingizwa kwenye bajeti ya 2017/18.
Miongoni mwa kata ambazo zimeondolewa katika ujenzi wa ofisi ni pamoja na Luchelele na Igoma ambazo zitaingizwa katika bajeti ya mwaka 2019/20.
Wakati Vicent akizungumza, meya huyo aliingilia kati na kuanza kuwatuhumu waandishi kwamba wanabagua na kwamba, huenda kuna mpango maalumu kwa waandishi hao bila kutaja mpango huo.
“Nyie waandishi hamfai kabisa, naomba mtupishe. Sitaki kuona waandishi wa habari humu ndani, mimi ndio mwenyekiti wa kikao hiki.
“Sitaki kuwaona humu ndani waandishi, haiwezekani mnabagua madiwani wengine huku wengine mnawarekodi mtakuwa mna mpango wenu wenyewe hivyo tupisheni humu,” amesema Meya Bwire.
Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba amewaambia waandishi kuwa, mwenye kikao chochote cha baraza ni meya hivyo watekeleza agizo la kutoka nje ya kikao hicho.
Leave a comment