BERNARD Membe, mgombea urais wa Tanzania kupitia ACT-Wazalendo, ameweka hadharani mambo manne yaliyosababisha kufukuzwa Chama Cha Mapindu (CCM). Anaripoti Faki Sosi, Lindi (endelea).
Membe alifukuzwa CCM tarehe 28 Februari 2020 akituhumiwa kukiuka miongozo na taratibu ya chama hicho tangu mwaka 2014.
Leo Jumanne tarehe 1 Septemba 2020, akihutumia mamia ya wananchi kwenye mkutano wa kampeni za urais uliofanyika uwanja wa Mpilipili Mjini Lindi, Membe amewaeleza wananchi hao wa kusini ikiwa ni mara ya kwanza kuzungumza mkasa huo kwenye mkutano.
Membe aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa Tanzania tangu mwaka 2007 hadi 2015 enzi za utawala wa Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete amesema, jambo la kwanza ni ubovu wa barabara za Kusini, “Tumechoka kutembea na mavumbi kana kwamba tunatoka mashambani kila siku.”
Pili, Membe ambaye ni Mshauri Mkuu wa ACT-Wazalendo amesema, ni dharau tunazofanyiwa watu wa Kusini, tunaonekana kama wajinga, watukanwe mashangazi zetu, hizo ni dharau ambazo hatupaswi kufanyiwi.
Tatu, Membe amesema, kilichomuondoa ni kunyimwa nafasi ya kugombea urais ndani ya CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu kwa kigezo kwamba Rais John Magufuli aachiwe amalize mhula wake wa pili ambao haupo kisheria au Kikatiba.
Nne, Membe amesema lililomfanya afukuzwe CCM ni namna Serikali ilivyoshusha thamani mazao ya biashara hususani Korosho ambalo ni zao muhimu kwa wakasi wa mikoa ya kusini.
Wakati huo huo, amesema mara atakapoingia madarakani atawarejesha mawakala wa ununuzi wa korosho maarufu kama Kangomba kwa kuwa hakuma uchumi wa biashara bika kuwepo mtu wa kati.
Membe amewasisitiza wananchi wa mikoa ya kusini kulima mazao ya biashara kwani atayasimamia mazao hayo kuhakisha yanauzwa kwa bei mzuri.
Kuhusu afya, Membe amesema, atasimamia ipasavyo upatikanaji wa bima ya afya ya magonjwa yasiyolipiwa na chini ya utawala wake italipiwa gharama zake kwa asilimia moja ya tatu na mgonjwa akifariki maiti itatolewa bure.
“Umesikia wapi maiti ikatozwa huu si uchuro,” amesema Membe ambaye amewahi kuwa mbunge wa Mtama mkoani Lindi.
Amesema kauli za uchumi wa kati ni za utani wenye kuumiza kwa kuwa wananchi hawana fedha.
Kuhusu ongezeko la mishahara kwa wafanya kazi, amesema serikali yake itaongeza mshahara kila mwaka “kuna watu hawajapandishwa mshahara miaka mitano, hajapandishwa vyeo chagueni Membe nitawapandishia mshahara.”
Akigusia suala la uvuvi amesema, Serikali yake haitabuguzi wavuvi na kwamba wavuvi hawatachomewa moto vitendea kazi vyao.
Kuhusu masoko ya mazoa ya biashara amesema, ataunda wizara maalum itakayokwenda nje kusaka masoko ya biasha za mazoa hayo.
Akizungumzia ya mahusiano ya Tanzania na mataifa mengine “Tutarudisha heshima ya Tanzania duniani, tutaanza upya urafiki na mataifa mengine.”
“Hatujawahi kuwa na uhasama na majirani zetu lakini siku hizi kila siku utasikia Rwanda wameondoka mara Kenya wamefunga mipaka yake,” amesema Membe.
Leave a comment