WABUNGE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ama wamemchoka Halima Mdee, mbunge asiye na chama bungeni au wamekerwa na kauli yake, aliyosema ‘kuna wabunge njuka.’ Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mdee alitumia neno wabunge njuka akimaanisha wabunge wapya ndani ya Bunge.
Wabunge hao wameeleza kukera na kauli ya Mdee ambaye tarehe 27 Novemba 2020, yeye na wenzake 18, walifukuzwa Chadema wakituhumiwa kwa usaliti kwa kujipeleka bungeni kuapishwa.
“Ombi langu kwa sisi tuliopewa dhamana na wananchi wa Tanzania, bila kujali vyama vyetu, bila kujali umeingilia mlango gani maana wapo wabunge hapa vyama vyao vimewakana,” amesema Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, alipokuwa akichangia mpango wa maendeleo wa miaka mitano 2021-2026.
Silaa amesema, “…msemaji hapa anasema ndege zimepaki, ndege haziruki kama kunguru. Tumenunua ndege Q400 za safari za ndani na Air Bus masafa marefu.”
Huku wabunge wakishangilia na Silaa akitaka kuendelea kudadavua, Spika Job Ndugai ‘aliingilia’ kati kwa kumshukuru Silaa kwa mchango wake.
Hata hivyo, Silaa alitaka kuendelea lakini Spika Ndugai akarejea tena maneno yale yale ya kumshukuru ‘asante sana,’ kwa maana ya kutaka Silaa akae chini.
Kauli ya Silaa ilipongezwa kwa idadi kubwa na wabunge wa CCM, ambao ndio waliwapongeza Mdee na kundi lake wakati walipoingia bungeni kwa mara ya kwanza.
Spika Ndugai akasemama na kusema “hilo ndiyo bungeni bwana, naona njuka wamechachamaa, wamekataa kabisa kuitwa njuka, Halima umechokoza mwenyewe, ndiyo raha ya mjengoni.”
“Mjadala ya moto kabisa na mwisho wa siku tutafika tu,” amesema Ndugai
Mdee alipata ‘shambulizi’ linguine kutoka kwa Godwin Kunambi, Mbunge wa Mlimba (CCM). Akikamilisha mchango wake alimuonya Mdee, aliyewahi kuwa mbunge wa Kawe.
“Kwanza nianze na lugha za kejeli, lugha za kuudhi na sisi wengine ni vijana pia, bado hata umri wa busara haujafika…., namuonya aache lugha za kejeli humu ndani ya bunge. Namuaonya tu, hamna njuka hapa, njuka maana yake nini?” amesema Kunambi huku wabunge wa CCM wakimshangilia.
“Amezungumzia suala la ATCL, ni huduma tu, anakuja hapa anatudanganya, tunampigia makofu tu,” amesema Kunambi
Baada ya Kunambi kumaliza kuzungumza,mmoja aliwasha kipaza sauti na kusema ‘taarifa, taarifa mheshimiwa spika, taarifa,” hata hivyo, Spika Ndugai alipuuza na kisha kusema “jamani tusikilizane, bahati nzuri hakuna taarifa, kwa hiyo tunaendelea.”
Leave a comment