MBUNGE wa Ulanga mkoani Morogoro, Goodluck Mlinga amelishauri Bunge kubadili kanuni ili Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani anapokiuka kanuni na sheria za Bunge, aondolewe. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mlinga ametoa wito huo leo tarehe 4 Aprili 2019 wakati akichangia mjadala wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu ombi lake la kulitaka bunge kuazimia kumuadhibu Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kwa kutohudhuria mikutano mitatu kutokana na kukutwa na hatia ya kulidharau bunge.
Mlinga amedai kuwa, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe ameshindwa kusimamia vyema wabunge wake ili wasivunje sheria za bunge, huku akimtuhumu kwamba, anaongoza kwa utoro bungeni.
“Juzi nilisema katika hili bunge tuna viongozi wetu, sisi CCM usipohudhuria vikao vitatu unaandikiwa barua, uki-miss behave- (ufifanya utovu), unaitwa kwenye kamati za vyama, hawa wenzetu viongozi wao wakikutana wakimaliza suala la kuchangishana fedha, hakuna habari nyingine, mbunge ahudhurie asihudhurie lwake,” amesema na kuongeza Mlinga.
“Inafika kipindi mpaka mbunge anafukuzwa bunge, kiongozi wao hajui, kiongozi wao mwenyewe ukihesabu katika vikao vinavyozidi 150 vya mwaka, vikao anavyohudhuria hata vikao 20 havifiki. Kwa wenzetu hawana kiongozi, ifike mahala tubadilishe kanuni kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani asipohudhuria vikao kadhaa, na yeye aenguliwe.”
Aidha, Mlinga ameshauri wadhifa wa uongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni upelekwe kwa CUF badala ya Chadema akidai kwamba, wabunge wa chama hicho hawana desturi ya kulidharau bunge pamoja na utoro.
“Wapewe hata CUF, leo hii tujiulize CUF kwa nini hawasimamishwi, kwa nini hawa miss behave bunge ,hawatoi lugha chafu, kwa nini ni wao tu, kuna chama cha ACT huku kwa nini hayawakuti.
“Mfano Lema wakati anafanya utumbo wake juzi na kiongozi wake wa upinzani yupo hasemi chochote, nilisema tubadilishe hata hizi kanuni hawa viongozi wao wawajibike kwa mambo wanayofanya wabunge wao,” amesema Mlinga.
Leave a comment