MBUNGE wa Viti Maalum asiye na chama bungeni, Cecilia Daniel Paresso, ameiomba serikali kudhibiti mfumo wa bei kubwa za bidhaa sokoni ili kupunguza gharama za maisha kupanda. Anaripoti Nasra Bakari, DMC…(endelea)
Ombi hilo limetolewa leo Jumatano, tarehe 2 June 2021, bungeni jijini Dodoma, wakati wa kipindi cha maswali na majibu.
Mbunge huyo amesema, gharama ya bei za bidhaa sokoni ni kubwa, kiasi kinachosababisha uchumi wa maisha kupanda.
“Je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti mfumuko mkubwa wa bei za bidhaa ulioanza tangu Desemba 2020, ambao umefanya gharama za maisha kupanda,” amehoji Paresso.
Akijibu swali hilo, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba amesema, mfumuko wa bei ulipanda kutoka asilimia 3.2 mwezi Desemba 2020, hadi kufikia asilimia 3.5 Januari 2021 na hii ilitokana na baadhi ya upungufu wa bidhaa sokoni.

Dk. Mwigulu amesema, aidha mfumo wa bei ulishuka kufikia asilimia 3.3 mwezi Februari 2021, ikiashiria bidhaa na huduma zilianza kupatikana kwa bei nafuu kulinganishwa na mwezi Januari 2021.
“Lengo la serikali ni kuhakikisha mfumuko wa bei unaendelea kubaki ndani ya wigo wa tarakimu moja kati ya asilimia 3.0 hadi 5.0. Lengo hili linaweza kufikiwa na mikakati mbalimbali ya serikali.
“Baadhi ya malengo hayo ni kuimarisha usambazaji wa chakula kutoka maeneo ya uzalishaji hadi katika maeneo ya walaji, kuimarisha usimamizi wa sera ya bidhaa na bajeti na kuboresha miundombinu ya barabara za vijiji ili kurahisisha usafirishaji wa mazao,” amesema Dk. Mwigulu
Leave a comment