RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewataka waliogombea ubunge na kukosa na sasa wameteuliwa kuwa wakuu wa mikoa (RC), kutofikiria ubunge na wasubiri wakati ufike. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Samia ametoa kauli hiyo leo Jumatano, tarehe 2 Juni 2021, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, wakati alipowaapisha makatibu tawala wa mikoa (RAS) na George Mkuchika, kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Kazi Maalum.
Miongoni mwa wakuu wa mikoa ambao waligombea ubunge ndani ya CCM katika uchaguzi mkuu uliopita ni; David Kafulila (Kigoma Kusini) na Omary Mgumba jimbo la Morogoro Kusini Mashariki.
Rais Samia amemteua Kafulila kuwa mkuu wa mkoa wa Simiyu na Mgumba kuwa mkuu wa mkoa wa Songwe.
“Wale wote waliogombea ubunge kama kina Mgumba na hamkufanikiwa kwa sababu hizi na hizi tukawakata, kawaida mawazo yenu yanakuwa kule mlikotoka, kafanyeni kazi, wakati ukifika tutapangana tu. Msiwasumbue waliopo,” amesema Rais Samia.
Ametumia fursa hiyo kuwataka kwenda kufanya kazi kwa ushirikiano na “mtafanikiwa tu kama mtafanya kazi na watu, mkienda kufanya kazi mkijiweka juu, hamtafanikiwa kwani wanasema mafanikio yako kwenye watu.”
“Mnakwenda kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, hata kama uwe umetoka chama kingine, wenye ilani mtawakuta kule, kuna chama kwenye mikoa, kuna chama kwenye wilaya. Nendeni mkafanyeni nao kazi,” amesema Rais Samia.
Ongera mama oo twakupongeza