MBUNGE wa Arumeru Magharibi wa chama tawala nchini Tanzania-CCM, Lembris Noah, amemuomba Rais wa Taifa hilo, Samia Suluhu Hassan, atimize ahadi ya ujenzi wa barabara jimboni kwake kwenda Hospitali ya Wilaya ya Arumeru, ili kuokoa maisha ya kina mama wanaotaka kujifungua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Noah ametoa ombi hilo asubuhi leo Jumapili, tarehe 17 Oktoba 2021, katika ziara ya kikazi ya Rais Samia mkoani Arusha.
Mbunge huyo wa CCM amesema, ubovu wa barabara hiyo umesababisha baadhi ya kina mama kujifungulia njiani.
“Tunaomba ujenge kilomita tatu za lami katika barabara inayotoka Arumeru Magharibi kwenda Hospitali ya Wilaya ya Arumeru, barabara hiyo ni mbovu sasa hivi kina mama wanajifungulia njiani. Juzi kuna mama amejifungulia katikati ya barabara. Ikikupendesha wale wamama wanalia chonde choinde,” amesema Noah.
Rais Samia amejibu maombi ya mbunge huyo akisema, Serikali yake itakaa na uongozi wa Arusha, ili kubainisha barabara za kipaumbele kwa ajili ya kuzijenga.
“Barabara ni kipaumbele changu kikubwa, tutachofanya ni kukaa na uongozi wa Mkoa wa Arusha na wilaya zake, tuangalie barabara zile zenye kipaumbele ndizo tutakazoanza shughulikia,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amesema Serikali yake imeongeza bajeti ya fedha na ujuzi katika wakala zinazoshughulika na ujenzi wa barabara, Wakala wa Barabara Tanzania (Tabaroads) na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini (TARURA).
“Mnajua barabara kuna maeneo mawili, Tanroads na TARURA kwa hiyo tutafanya kipaumbele. Lakini tunachofanya tumeongeza uwezo mkubwa TARURA wa fedha na utaalamu ili barabara za ndani zinazolalamikiwa ziweze kutengenezwa kiwango cha changarawe,” amesema Rais Samia.
Leave a comment