Saturday , 27 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Mbowe amaliza utetezi, Msigwa aanza 
Habari za SiasaTangulizi

Mbowe amaliza utetezi, Msigwa aanza 

Spread the love

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, ameiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwamba chama chake hakina dhamira ya kushika madaraka kwa vurugu wala umwagaji wa damu. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).

Akitoa utetezi wake mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Thomas Simba, jijini Dar es Salaam jana, tarehe 29 Novemba 2019, Mbowe alisema, chama chake hakijihusishi na vurugu na wala hakina makundi ya aina hiyo. 

Alikuwa akijibu swali la iwapo sera za chama chake, zinahamasisha vurugu, watu kutembea na silaha barabarani, na kupandikiza  chuki kwa jamii na uvunjifu wa amani.

Alitoa kauli hiyo, wakati akikamilisha utetezi wake. Alikuwa akihojiwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi.

Mbowe na viongozi wengine nane wa chama hicho, wanakabiliwa na mashitaka 13 ya jinai, likiwamo kufanya maandamanokinyume cha sheria, kutoa maneno ya uchochezi na kufanya kusanyiko lisilo halali na kusababisha kifo cha Mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwelina Akwelin.

Washitakiwa wengine kwenye kesi hiyo Na. 112 ya mwaka 2018, ni pamoja na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Vicent Mashinji; na manaibu katibu mkuu, John Mnyika Bara na Salum Mwalim Zanzibar.

Katika orodha hiyo, wamo pia mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche; Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya; Mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko; Mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa.

Akijibu swali iwapo kuna ibara au kifungu cha sheria; na au Katiba, kinachoruhusu mtu au chama cha siasa kuchukua nchi kwa kumwaga damu, mwenyekiti huyo wa Chadema alidai, “sifahamu.”

Kuhusu iwapo katika miaka 15 ya ubunge wake, hakuwahi kukutana na kifungu au ibara ya sheria na Katiba inayomruhusu mtu au chama kuchukua madaraka kwa kupitia utaratibu wa kubeba marungu, Mbowe alidai, hajawahi kukutana na kifungu cha aina hiyo.

Awali akiongozwa na wakili wake wa utetezi, Peter Kibatala, mwanasiasa huyo aliieleza mahakama hiyo kuwa chama hicho kinakusudia kuchukua madaraka kwa kupitia sanduku la kura na siyo kushika madaraka kwa kutumia maguvu.

Alidai kuwa haijawahi kuwa dhamira ya Chadema kuhamasisha chuki, vurugu na watu kutembea na silaha barabarani. Mbowe alimaliza kutoa utetezi wake jana, jambo ambalo lilimpa nafasi Mchungaji Msigwa kuanza kujitetea.

Akiongozwa na wakili wake, Peter Kibatala, Mchungaji Msigwa alidai, siku ya tarehe 16 Februali, alifika kwenye viwanja vya Buibui baada ya kupigiwa simu na mratibu wa kampeni na mtu aliyemtaja kwa jina la Benson Kigaila. Alisema alifika Dar es Salaam, kutokea nyumbani kwake Iringa, siku moja kabla.

Msigwa ameieleza mahakama kuwa hakuhusika kwenye kosa la kwanza la kukutana na washtakiwa wengine na kula njama za kufanya maandamano kwa kuwa yeye hakuwahi kukutana na mtu yeyote mahala popote kupanga jambo hilo.

Alipoulizwa kuhusika kwake kwenye kosa la pili la kufanya kusanyiko lisilohalali, Msigwa alidai kuwa shitaka hilo ni la uongo na linalenga kuipotezea mahakama muda wake.

Kuhusu shitaka la nne la kufanya maandamano kinyume cha sheria, ambako anadaiwa kuwa alihamasisha watu kwenda kwenye Ofisi za Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondini kufuata barua za mawakala wao, haraka alisema, “shitaka hilo nalo ni la uongo na la kutunga.”

Alipoulizwa kuhusu ufahamu wake kuhusiana na kifo cha Akwelina Akwiline, Mchungaji Msigwa alidai, alikisikia na kuona kwenye vyombo vya habari.

Msigwa alidai pia kwamba alimsikia Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa akieleza kuwa wanawashikilia asakari wawili kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya Akwelina.

Aidha, Msigwa aliendelea kuileza mahakama kuwa alimsikia pia mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Kamanda Simon Sirro, akieleza kuwa Polisi wamefaya makosa kwenye tukio hilo.

Kibatala amemuuliza Msigwa kuhusu kauli ya kusema kuwa tukamchinje Magufuli, alioneseha kitambulisho cha mpigakura na kueleza kuwa hiko anakiita kichinjio; na kwamba hakina maana ya kumchinja mtu kumtoa damu ni kwenye sanduku la kupigakura.

Hakimu Simba aliahirisha shauri hilo mpaka tarehe 2 Desemba 2019, ambapo itaendelea kwa siku tano mfululizo.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

ACT: Waongoza watalii wapate maslahi yao inavyostahili

Spread the loveCHAMA cha ACT-Wazalendo kimeitaka serikali kuhakikisha inasimamia maslahi stahiki ya...

Habari za SiasaTangulizi

Prof. Lipumba ajitosa kuviunganisha vyama vya siasa Burundi

Spread the love  MWENYEKITI wa Kituo Cha Demokrasia Tanzania (TCD), Prof. Ibrahim...

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

error: Content is protected !!