GHARAMA kubwa za matibabu zilizowekwa na Mfuko wa Bima ya Afya nchini (NHIF), zitaumiza wengi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 29 Novemba 2019 na Dorothy Semu, Katibu Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, kwenye ofisi kuu ya chama hicho Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.
Amesema, maboresho yaliyofanywa na kutangazwa na mfuko huo, yanaendeleza matabaka na kwamba, gharama zilizowekwa ni kubwa kulingana na hali halisi ya wananchi.
“Kwa maamuzi haya, serikali imeamua kugeuza NHIF, kutoka kuwa Bima ya Umma kwenda kuwa Bima Binafsi. Duniani kote kuna Bima aina mbili – Bima binafsi na Bima ya Umma. Kiwango cha malipo ya kila mwaka kwa kila mtu ni tofauti.
Tunajua ni kwanini serikali ya CCM, imeamua kuanza biashara ya Afya ya Watanzania. ACT- Wazalendo inashauri kuwa, huduma ya vifurushi vipya vya NHIF isimamishwe mara moja.
“…na ili kupunguza matumizi makubwa ya rasilimali fedha, ni muhimu kama nchi kuwekeza katika mfumo wa afya unaolenga kuboresha afya ya msingi kwa wananchi wake,” amesema.
NHIF imezindua vifurushi vipya na gharama za matibabu, huku ikitenganisha umri na kiwango cha fedha kitacholipiwa kulingana na aina ya gharama.
Mfuko huo umeeleza watu wenye umri wa kuanzia 18 – 35 watalipia Sh. 192,000 kwa mwaka kupitia kifurushi cha Najali Afya Premium, kifurushi cha Wekeza Afya Sh. 384,000 na Sh. 516,000 kwa kifurushi cha Timiza Afya.
Katika vifurushi vingine, gharana zinaongezeka na hata kufikia Sh. 984,000 kwa mwaka jambo ambalo linapingwa na chama hicho.
Semu amesema, gharama zilizowekwa katika viwango hivyo, haziwezi kugharamiwa na watu wa hali ya kawaida, jamboa ambalo linaongeza matabaka nchini.
Amekosoa utaratibu wa vifurushi kwamba, ugonjwa umechukuliwa kama jambo la hiyari akisema “binadamu hachagui kuumwa au aina ya ugonjwa ambao anapaswa kuumwa.”
Ameitaka serikali kutofanya ugonjwa kama mtaji wa kujipatia fedha na badala yake, iwajibike katika kuhudumia wananchi kwa gharama zinazoweza kubebeka.
Leave a comment