SERIKALI ya Tanzania, imeziagiza kamati za kutokomeza ukatili wa kijinsia zishirikiane na vyombo vya dola, kutokomeza mauaji yanayosababishwa na migogoro ya kifamilia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Alhamisi, tarehe 3 Februari 2022, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Dk. Dorothy Gwajima, wakati akijibu swali la nyongeza Mbunge wa Iringa Mjini (CCM), Jesca Msambatavangu, aliyehoji wizara hiyo imejipangaje kutokomeza mauaji hayo.
“Kuhusu mauaji na vitendo vya ukatili vinavyoendelea kwenye jamii yetu, tunao mkakati wa kutokomeza ukatili kwa wanawake na watoto, Mpango wa Taifa uliozinduliwa 2017/18 na unakwenda mpaka 2021/22,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwajima amesema “ambao umeandaa kamati kwenye ngazi ya kijiji zinaongozwa na wenyeviti wa serikali za vijiji, mtaa, kata, halmashauri mpaka Taifa na mkoa ukiwemo, sasa kamati hizi. Tumeshazipelekea malekezo.”
Waziri huyo wa maendeleo ya jamii, amesema kamati hizo zina majukumu ya kuripoti viashiria vya mauaji hayo katika vyombo vya dola.
“Tuankwenda kuadhimisha siku ya kupinga ukeketaji tarehe 6 Februari hii, ni fursa ya kuziamsha kamati zote zifanye kazi yake zikitekekleleza majukumu yake yaliyomo kwenye huo muongozo,” amesema Dk. Gwajima na kuongeza;
“Tutaweza kudhibiti huo ukatili unaotokea kwenye jamii, kwa kuona viashiria husika na kuvitolea taarifa katika vyombo husika vinavyoshughulika na uhalifu.”
Miongoni mwa mauaji hayo, ni yale yaliyotokea mkoani Kigoma, ambapo Amos Buhaga (68), aliuawa tarehe 2 Januari 2022, kwa kujeruhiwa na kitu chenye ncha kali kisogoni akituhumiwa kwa imani za kishirikina.
Tukio lingine ni la Helman John, anayedaiwa kumuuwa mama yake Celina William (63), tarehe 5 Januari 2022, akimdai fedha kiasi cha Sh. 300,000.
Leave a comment