JUMLA ya Marais wa nchi nne pamoja na marais wastaafu watatu wamehudhuria sherehe za maadhimisho ya miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara zilizofanyika katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam leo tarehe 9, Disemba 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Marais hao ni wa Kenya, Uhuru Kenyatta; Rwanda, Paul Kagame; Msumbiji, Felipe Nyusi pamoja na visiwa vya Comoro, Azali Assouman.
Aidha, marais wengine ambao hawakufika wametuma wawakilishi mbalimbali ikiwamo mawaziri.
Marais wastaafu waliohudhuria sherehe hizo ni Rais mstaafu wa Malawi, Joyce Banda; Rais mstaafu wa Msumbiji, Joachim Chisamo na Rais Mstaafu wa Botswana, Festus Mogae.
Katika maadhimisho hayo yaliyopambwa na halaiki ya wanafunzi zaidi ya 600 pamoja na gwaride la vikosi vya ulinzi na usalama Jeshi la Uhamiaji, Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta ndiye aliyekuwa mgeni rasmi.
Akitoa utambulisho wa wageni hao, Rais Samia Suluhu Hassan amesema Kenyatta ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki pia amewasili nchini kwa ziara maalumu ya kiserikali.
“Kwa hiyo tutakuwa naye pia kesho lakini kule Kenya shamrashamra na vuguvugu la uchaguzi limeanza kwa hiyo Rais Kenyatta, tutakuwa naye mara ya mwisho kuwa kama mkuu wa nchi katika sherehe za aina hii. leo kama mkuu wa nchi,” amesema.
Viongozi wengine waliohudhuria sherehe hizo ni Makamu wa Rais wa Burundi, Prosper Bazombaza; Waziri Mkuu Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),, Jean-Michel Sama Lukonde na Naibu Waziri Mkuu Eswatini, Themba Nhlanganiso Masuku.
Wengine ni Spika wa Bunge la Juu la Oman, Sheikh Abdulmalik Abdullah Ali al Khalili akimwakilisha Mfalme wa Oman; Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Musa Faki Mahmad; Waziri Mkuu Uganda, Dk. Ruhakana Rugunda mjumbe maalumu wa Rais Yoweri Museveni Rais wa Uganda.
Pia Waziri wa masuala ya kimataifa ya Jamhuri ya Botswana, Dk. Lemogang Kwape akimwakilisha Rais wa Botswana; Waziri wa Ulinzi na masuala ya Veterani wa Zimbabwe, Oppah Muchinguri-Kashiri; Naibu Waziri Ushirikiano wa Kimataifa Afrika kusini, Naledi Pandor.
Amewatambulisha pia Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu, Jaji Iman Abood; Katibu Mkuu wa jumuiya ya afrika mashariki, Dk. Peter Mathuki; Balozi wa Jmahuri ya Namibia – Tanzania, Lebbius Tangeni Tobias; Naibu Mkurugenzi wa Operesheni ya Mfuko wa Kuwait, Ghanem Sulaiman Al Ghenaiman.
“Hawa ndio waliotuunga mkono kwenye sherehe zetu leo, nichukue fursa hii kwa niaba ya Watanzania kuwashukuru sana kaka na dada zetu waliokuja kutuunga mkono na huu ndio umoja wa kanda zetu ndio umoja wa Afrika,” amesema.
Pia amewashukuru wananchi wote kwa kuja uwanjani na kushikiri kwa kikamilifu maadhimisho yetu kwa wiki nzima ya maadhimisho ya sherehe hii.
Awali Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mandalizi ya maadhimisho hayo, amesema hotuba ya jana ya Rais Samia ilikuwa ya msisimko wa aina yake.
“Ilikuwa kiashirio kuanza rasmi kwa safari ya kuelekea maadhimisho ya miaka 60 Uhuru wa Tanzania Bara na miaka 59 ya Jamhuri
“Wananchi nyote mtakubaliana name kwamba hotuba ya Rais Samia imekuwa chachu ya kuendelea kuimnairsha amani, mshikamano na umoja wa kitaifa huku ikitukumbusha wajibu wa kuleta tafakuri ya wapi tulipotoka, wapi tulipo na wapi tunataka kufika,” amesema.
Leave a comment