MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) – Taifa, Philiph Mangula amesema, wasiasa ndio wamekuwa chanzo cha viashiria vya kuteteresha amani ya nchi. Anaripoti Christina Haule…(endelea).
Kutokana na hali hiyo, amewataka viongozi wa dini nchini, kutokaa kimya pale viashiria vya kutoweka kwa amani vinapotokea.
Ametoa kauli hiyo tarehe 17 Novemba 2019, kwenye maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 25 tangu kusajiliwa kwa Kanisa la Calvay Assemblies of God. Hafla hiyo iliyofanyika mjini Morogoro.
Mangula amesema, wanasiasa wamekuwa chanzo cha kuvuruga amani na machafuko kwa kuwa, hutafuta madaraka kwa njia mbalimbali hata kuhusisha rushwa.
“Mfano mzuri ni siasa nchini ya jirani,,,, Iddi Amini ambaye sasa hivi ni marehemu, alitumia hila na kusababisha vita kubwa miaka ile iliyoua wengi, chanzo kikubwa uvunjifu wa amani, jambo ambalo halipendezi,” alisema.
Na kwamba, viongozi wa dini hawana budi kutambua kuwa, wao ni jeshi kubwa ambalo pia linategemewa katika kuhubiri na kuilinda amani ya nchi.
“Taifa letu bila ninyi viongozi wa dini litayumba, bila roho za watu kumuona Mungu ndiye, tutayumba, hatutaweza,” alisema
Aidha aliwataka kutambue, kuwa Uhuru wa kuabudu na yote wanayofanya ni kwasababu nchi ina Amani, na kwamba ni wajibu wao kama kanisa kuhakikisha wanaendelea kuwaombea wanasiasa pamoja na kuombea amani ya nchi ili iendee kudumu.
Askofu Mkuu wa kanisa hilo Morogoro, Dk. Dunstan Maboya alisema, wanatambua kuwa asiyefanya kazi na asile, hivyo wao kama Kanisa, wanahakikisha wanawainua kiuchumi watumishi wao kwa elimu ya ujasiliamali wakiwemo wachungaji na maaskofu ili wasiingie kwenye utapeli.
“Ibrahimu ambaye ni baba wa Imani alikuwa na mashamba, Yohana alikuwa anatengeneza ngozi, watumishi wa Mungu wanapaswa kuwa na shughuli ambazo zinawaingizia kipato ili kuepuka kuingia kwenye utapeli,” alisema
Askofu Maboya alisema, watumishi wa Mungu ambao wanaingia kwenye utapeli, ni kwasababu wameshindwa kusimama kwenye zamu zao na kufuata mafundisho wanayopewa.
Awali, Katibu Mkuu Msaidizi, Askofu Martin Mlata alisema, Kanisa hilo ni mdau mkubwa wa maendeleo, na kwamba limekuwa mstari wa mbele katika kuandaa miongozo ya shughuli za kijamii ikiwemo Elimu ya ujasiliamali, afya, kilimo na ufugaji.
Leave a comment