MWALIMU Mkuu Mstaafu wa Shule ya Msingi Bwigiri Wasioona, Chamwino mkoani Dodoma, Sylivavus Hosea ambaye ni mlemavu wa macho, amemwomba Rais John Magufuli kuangalia namna ya kuteua wabunge watatu walemavu katika nafasi zake 10 za uteuzi. Anaripoti Dandson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na mtandao huu tarehe 17 Novemba 2019 amesema, pamoja na kuwapo wabunge wenye ulemavu bungeni, bado kuna nafasi za uwakilishi ambazo zinakosekana bungeni ikiwemo walemavu wa macho na wasiosikia (viziwi).
Kutokana na hali hiyo, amesema kama ikimpendeza Rais Magufuli na mwingine yeyote katika uongozi wake, aone jinsi ya kuchagua makundi hayo matatu yenye ulemavu kwa maana ya watu wenye ulemavu wa viungo, viziwi pamoja na wasioona.
Mbali na hilo amesema, jambo ambalo angefurahi kuona ni pale wabunge wangeweza kupeleka mswada bungeni ambao unawataka watu wenye ulemavu, kutokana na jumuiya za vyama vyao kama yalivyo makundi mengi ya vijana na wanawake.
“Zamani ilikuwa ngumu sana akina mama kugombea ubunge jimboni au udiwani katika kata, lakini kutokana na kupatiwa nafasi ya viti maalum na kufanya vizuri. Wameweza kuaminika hata kugombea majimbo na kufanikiwa kupenya na wakati mwingine kuwashinda wanaume,” amesema.
Leave a comment