MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, imetengua adhabu ya kifungo cha miezi sita alichohukumiwa mbunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika jimbo la Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, maarufu kwa jina la Sugu. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Katika umuazi wake aliyeutoa leo, tarehe 11 Oktoba 2019, Jaji wa Mahakama Kuu, John Utamwa, amesema kuwa mahakama yake imebaini kuwapo kwa mapungufu makubwa ya kisheria yanayoondoa uhalali wa kifungo hicho.
Jaji Utamwa ametaja makosa hayo kuwa ni pamoja na Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Mbeya, kushindwa kuwasomea watuhumiwa mashtaka katika hatua ya usikilizaji wa awali – Preliminary Hearing (PH).
Sugu na aliyekuwa mshitakiwa mwenzake, Emmanuel Masonga, walitiwa hatiani na Michael Mteite, ambaye alikuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mbeya na hivyo kuwaamuru kutumikia kifugo cha miezi sita, tarehe 26 Februari 2018.
Walituhumiwa hao wawili, walidaiwa kutoa maneno ya “kumfedhehesha Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk. John Pombe Magufuli.”
Mahakama ilielezwa na upande wa mashitaka kuwa Sugu na Masonga, walitoa kauli hiyo, wakati wakihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Lwanda, Nzovwe, jijini Mbeya, 31 Desemba 2017.
Akisoma maamuzi ya rufaa hiyo Na. 29 ya mwaka 2018, iliyowasilishwa na Sugu kupitia mawakili wake, Peter Kibatala na Faraji Mangula, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, amesema kuwa Jaji Utamwa ameridhika kuwa katika shauri lililowatia hatiani mbunge huyo na mwenzake, kulikuwa na “makosa yasiyotibika.”
Naibu Msajili amesema, Jaii Utamwa ameeleza kuwa hakubaliani na hoja za upande wa Serikali ambao ni wajibu Rufaa, kwamba mapungufu hayo yanatibika.
Amesema, makosa hayo yanaathiri mwenendo mzima wa kesi iliyosababisha mahakama kuwahukumu kifungo waomba rufaa.
Kufuatia makosa hayo makubwa katika mwenendo wa kesi za jinai, Naibu Msajili amesema, “Jaji Utamwa ametengua hukumu, mwenendo mzima wa kesi na adhabu ya kifungo waliyohukumiwa Sugu na Masonga.”
Sugu na mwenzake, waliishi gerezani kwa muda wa siku 73 kati ya siku 120 walizopaswa kutumikia adhabu yao ya miezi sita, kufuatia kunufaika na msamaha wa rais, tarehe 10 Mei mwaka 2018.
Leave a comment