BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, limemuomba Rais John Magufuli kujenga reli ya treni ya abiria ya mwendo kasi kuanzia Dodoma mjini hadi mji mdogo wa Kibaigwa mkoani humo, anaandika Dany Tibason.
Madiwani hao wamesema ni bausara reli hiyo kufika Kibaigwa ambako kuna soko kubwa la mahindi badala ya kuishia Bwigiri wilayani Chamwino ili kurahisisha wafanyabiashara wa mahindi kusafirisha mizigo yao kwa urahisi.
Wakizungumza katika kikao cha Baraza hilo Madiwani hao walisema ujenzi wa reli hiyo hadi Kibaigwa utakuwa ni faraja kwa wananchi hususani wafanyabiashara wanaopeleka mazao katika soko la Kibaigwa.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, White Zuberi amesema soko la Kibaigwa lina wafanyabiashara wengi kutoka maeneo mbalimbali katika mkoa wa Dodoma na ambao wamekuwa wakipata shida kusafirisha mazao yao kuelekea katika soko hilo.
“Mheshimiwa Rais Magufuli ameahidi kujenga reli ya treni ya abiria kutoka Dodoma mjini hadi Bwigiri, lakini na sisi wanakongwa tunamuomba rais kujenga reli hiyo hadi Kibaigwa ambako kuna soko kubwa la mahindi ili kusogeza karibu huduma ya usafiri kwa wafanyabiashara wanaofika sokoni hapo,” amesema Zuberi
Pia Zuberi amesema reli hiyo itakapofika katika mji mdogo wa Kibaigwa itarahisisha usafiri kwa wananchi wa kawaida kwa kuwa hivi sasa kuna shida ya usafiri kati ya hapo na Dodoma mjini.
Leave a comment