SERIKALI imetakiwa kuweka mikakati ya kudhibiti ajali za barabarani zinazosababishwa na uzembe wa baadhi ya madereva wa pikipiki (bodaboda), ili kunusuru maisha ya wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 5 Februari 2024, bungeni jijini Dodoma na Naibu Spika wa Bunge, Mussa Zungu baada ya Mbunge wa Shaurimoyo, Ally Juma Mohamed (CCM) kuhoji Serikali ina mkakati gani kudhibiti ajali za bodaboda zinazogharimu maisha ya wananchi wengi.
“Suala la bodaboda ni kero kubwa hasa kwenye utumiaji wa sheria za barabarani, mimi ni mtetezi mkubwa sana wa bodaboda lakini matumizi yao kwenye barabara yanakatisha tamaa lazima muwe na mkakati maalum wa kudhibiti ajali ambazo wanazifanya,” amesema Zungu na kuongeza:
“Lazima muwe na sheria kali za kuwadhibiti na hata kuwasimamisha sababu Muhimbili ukienda MOI sasa hivi asilimia 90 ni vijana.”
Awali, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Jumanne Sagini, amelisema Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ya kudhibiti ajali za bodaboda ikiwemo kutoa elimu na kutumia sheria kuwaadhibu wanaobainika kukiuka sheria za barabarani.
Leave a comment