WILLIAM Lukuvi, Waziri wa Ardhi Nchini, amekemea vitendo vya uonevu vinavyofanywa na viongozi wa serikali za mitaa kwa kushirikiana na matapeli kuwanyonya wananchi, anaandika Irene Emmanuel.
Akizungumza leo katika eneo la Kimara, Kilungule wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, alipokabidhi hati 4000 za ardhi kwa wakazi wa eneo hilo, amewataka viongozi wa serikali za mitaa kuacha kutumia vyeo vyao vibaya.
“Baadhi ya viongozi wa mitaa mnatumia vibaya sana vyeo vyenu, mnauza mali za maskini, mnaotoa taarifa kwa matapeli kwamba mwenye kiwanja hiki kafa alafu mnatoa vibali wakati mnajua eneo hili ni bwana fulani na wakati ananunua mlitia sahihi.” amesema Lukuvi.
“Kesi nyingi ninazoona unakuta mtu amevamiwa shamba lake, lakini huyo mvamizi amesaidiwa na mwenyekiti wa mtaa yuleyule aliyetia sahihi kumuuzia mtu mwingine, hiyo tabia lazima ikome.” anaongeza.
Lukuvi, amewataka viongozi wa wilaya kufanya ukaguzi ili kuhakikisha kuwa sheria inafuatwa katika umiliki wa viwanja na ujenzi na siyo kujenga kiholela.
Leave a comment